Joy FM
Joy FM
14 May 2026, 10:55

Halmashauri ya Mji wa Kasulu mkoani Kigoma imeanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa shedi mpya kwa ajili ya wafanyabiashara wa mchele katika Soko la Sofya, mradi unaotarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi milioni 59.
Biashara ni shughuli muhimu inayosaidia kukuza uchumi wa mtu binafsi na taifa kwa ujumla na wafanyabiashara wengi hasa wa masoko na maeneo ya wazi hukabiliwa na changamoto mbalimbali kama mvua, jua kali na ukosefu wa sehemu salama za kufanyia biashara
Na Mwandisi wetu
Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Mwl. Vumilia Simbeye, amesema kuwa ujenzi wa shedi hiyo unalenga kuboresha mazingira ya biashara kwa kuwatoa wafanyabiashara kwenye vibanda vidogo vya sasa litakalowawezesha kufanya shughuli zao kwa uhuru na katika mazingira bora zaidi.
Katibu Msaidizi wa Soko la Sofya, Gibson Isaac, amesema hatua hiyo ya halmashauri kuboresha miundombinu ya soko itafungua fursa mpya za biashara na kuongeza ufanisi kwa wafanyabiashara mara baada ya kukamilika kwa jengo hilo na kuongeza mapato katika halmashauri hiyo.

Baadhi ya wafanyabiashara wa mchele katika soko hilo wameipongeza halmashauri kwa kuanzisha mradi huo, wakisema kuwa shedi mpya itawawezesha kufanya biashara katika eneo safi, salama na lenye hadhi inayostahili kwa bidhaa za chakula.

Aidha, wafanyabiashara hao wameiomba serikali kuhakikisha ujenzi wa mradi huo unakamilika kwa wakati kabla ya kuanza kwa msimu wa pili wa mvua. Pia wamependekeza kuboreshwa kwa huduma muhimu sokoni hapo ikiwemo upatikanaji wa nishati ya umeme pamoja na mifumo bora ya majitaka.
Mradi huo unatajwa kuwa sehemu ya juhudi za Halmashauri ya Mji wa Kasulu katika kuboresha mazingira ya biashara na kuinua shughuli za kiuchumi kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati ndani ya Mji huo.