Joy FM
Joy FM
13 June 2026, 20:27

Mkuu wa Wilaya Kasulu Kanali Isaac Mwakisu amesema Mkoa wa Kigoma una fursa nyingi za kiuchumi ambazo zinaweza kutumiwa na kuwanufaisha wananchi
Na Sadick Kibwana
Waumini wa dini ya Kikristo Mkoani Kigoma wametakiwa kuchangamkia fursa za kiuchumi zinazowazunguka ili kukuza vipato vyao na kujiletea maendeleo.
Rai hiyo imetolewa wakati wa kongamano la fursa za kiuchumi kwa vijana lililoandaliwa na Vituo vya Huduma ya Mtoto na Kijana, Klasta ya Kasulu na Kigoma Kaskazini, lililofanyika katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Akizungumza kwenye kongamano hilo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro, Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Isaac Mwakisu amesema mkoa huo una fursa nyingi za kiuchumi ambazo zikitumiwa vizuri zitamsaidia kila mmoja kujikwamua kimaisha.
Aidha, Kanali Mwakisu amewasihi washiriki wa kongamano hilo kuongeza mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia sambamba na jitihada za kukuza uchumi.

Naye Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Magharibi Kati (Kasulu), Jackson Mushendwa, amekiri kuwa kongamano hilo limekuwa chachu ya kupata maarifa mapya ya kiuchumi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Watendakazi wa Klasta ya Kigoma Kaskazini amebainisha kuwa lengo kuu la vituo hivyo vya maendeleo ni kuwaunganisha na kuwaandaa watoto ili waje kuzitumia fursa za kiuchumi.
Nao baadhi ya watoto wanaopata huduma katika vituo hivyo wameeleza namna walivyofaidika na mafunzo hayo.

Kongamano hilo ni la kwanza kufanyika likiunganisha klasta za Kigoma Kaskazini na Kasulu, ambapo limeongozwa na kauli mbiu isemayo: “Tumia fursa zinazokuzunguka, tokomeza ukatili dhidi ya watoto.”