Joy FM
Joy FM
9 September 2024, 15:21

Wanawake Mkoani Kigoma wameshauriwa kujitokeza kushiriki na kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kwenye jamii hasa katika uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu.
Na Luca Hoha – Kigoma Dc
Kuelekea uchaguzi wa Serikali za mitaa utakaofanyika Novemba 27 mwaka huu na uchaguzi mkuu hapo mwakani, Wanawake Mkoani Kigoma wametakiwa kujitokeza kushiriki kikamilifu kuwania nafasi mbalimbali za uongozi.
Hayo yameelezwa katika hafla yauzinduzi wa mradi wa kuhamasisha usawa wa kijinsia kushiriki kwenye siasa na uongozi unaoratibiwa na shirika lisilo la kiserikali la LEGAL AID SHARE AND CARE FOR ALL yani LASCA linalojihusisha na masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kutoa msaada wa kisheria na kupinga ukatili wa kijinsia lililopo Wilaya ya Kigoma
Afisa maendeleo ya jamii wilaya ya kigoma ambaye pia ni kaimu mratibu wa mashirika yasiyo ya kiserika George Vansauli ametumia nafasi hiyo kuwataka wanawake kujiamini kuwa wanao uwezo wa kuongoza, huku akiitaka jamii kuacha mfumo dume wa kuwakandamiza wanawake katika masuala ya uongozi na siasa.
Kwa upande wake, mratibu wa mradi huo kutoka shirika la LASCA lililopo Wilaya ya Kigoma John Kamaliza Ntabagala amesema wameamua kutekeleza mradi huo kwa sababu asilimia kubwa ya wanawake wamekuwa hawajitokezi kwenye masuala ya siasa kutokana na sababu mbalimbali za kijamii ikiwemi mila na desturi zinazowakandamiza wanawake.
Nao baadhi ya wanawake ambao wameshiriki uzinduzi wa mradi huo wamesema wamehamasika kushiriki kwenye masuala ya uongozi na siasa na kutaja baadhi ya majukumu yanayowafanya wasishiriki ikiwemo majukumu ya familia.