Joy FM
Joy FM
15 May 2026, 15:27

Mikopo ni mojawapo ya njia muhimu zinazosaidia maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika jamii kwa makundi tofauti ya watu ili kuwawezesha kujiletea maendeleo na miongoni mwa makundi yanayonufaika sana na mikopo ni wanawake, vijana, na watu wenye ulemavu
Na Hagai Ruyagila
Zaidi ya shilingi milioni 214 zimetolewa kwa vikundi 17 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma kupitia mpango wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Serikali kwa halmashauri mbalimbali nchini.
Mikopo hiyo ni kwa robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026. Akizungumza katika hafla hiyo ya kukabidhi mikopo hiyo kwa vikundi vilivyonufaika, Mgeni rasmi ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Kasulu Mjini Prof. Joyce Ndalichako amewataka wanufaika kuzitumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa, kurejesha mikopo hiyo kwa wakati na kuhakikisha vikundi vinaendelea kuwa na nidhamu ya fedha ili wananchi wengine waweze kunufaika na mpango huo.

Awali, akisoma taarifa ya utoaji wa mikopo hiyo, Mkuu wa divisheni ya Maendeleo ya jamii katika Halmashauri ya Mji Kasulu, Nurfus Aziz, amesema hiyo ni awamu ya pili ya utoa wa mikopo kwa mwaka wa fedha 2025/2026, akibainisha kuwa halmashauri hiyo tayari imetoa zaidi ya shilingi milioni 300 kwa vikundi mbalimbali.

Afisa maendeleo ya jamii kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa wa Kigoma, Minza Edward amesema baadhi ya wananchi wamekuwa wakichukua mikopo hiyo na kuitumia tofauti na malengo yaliyoainishwa katika maandiko yao, hali inayosababisha migogoro kati yao na serikali.
Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wamesema watazitumia fedha hizo kwa ufanisi ili ziweze kuwasiaidia kukuza shughuli zao za kiuchumi na kuboresha maisha ya familia zao.
