Joy FM
Joy FM
15 April 2026, 12:53 pm

Elimu ya fedha ni muhimu sana kwa vikundi vya kuweka na kukopa kwa sababu inasaidia wanachama kusimamia fedha zao kwa ufanisi na kuepuka hasara
Na Hagai Ruyagila
Serikali imeendelea kutoa elimu ya kifedha pamoja na mwongozo wa namna sahihi ya kujisajili kwa vikundi vya kuweka na kukopa katika Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma, ikiwa ni jitihada za kuwawezesha wananchi kupata mikopo katika taasisi zilizo salama na kuepuka changamoto za ulipaji.
Akizungumza na wanachama wa vikundi mbalimbali vya kuweka na kukopa pamoja na Kusaidiana katika Kata ya Heru Juu, Afisa Maendeleo ya jamii Halmashauri ya Mji Kasulu, eneo la uratibu wa vikundi vya kijamii na mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali, Gabriel Milombetse, amesema elimu hiyo inalenga kuwajengea uwezo wananchi katika usimamizi bora wa fedha pamoja na kuhakikisha wanajiunga na vikundi vilivyosajiliwa kisheria.

Kwa upande wake, Mwezeshaji wa Kata ya Heru Juu, Salum Mwingereza, amesema wako tayari kutoa msaada wakati wowote kwa vikundi vinavyohitaji kusajiliwa ili viweze kutambuliwa kisheria na kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza.

Baadhi ya wanavikundi waliopata elimu hiyo ya fedha pamoja na kusajili vikundi vyao wameishukuru serikali kwa kuwapatia mafunzo hayo, wakieleza kuwa yamekuwa na mchango mkubwa katika kuboresha uelewa wao wa masuala ya kifedha.
