Joy FM
Joy FM
22 July 2026, 09:41

Ukusanyaji wa mapato ni nguzo muhimu katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla na mapato yanayokusanywa na serikali kuu na mamlaka za serikali za mitaa kupitia kodi, ushuru na vyanzo vingine huwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayowanufaisha wananchi
Na Hagai Ruyagila
Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma imefanikiwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa zaidi ya asilimia 5 katika mwaka wa fedha 2025/26 baada ya kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 4 kutoka vyanzo mbalimbali vya mapato.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Mji Kasulu Mwl. Vumilia Simbeye wakati akizungumza na vyombo vya habari nakueleza kuwa halmashauri hiyo imekuwa ikifanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa kila mwaka hali inayosababisha kuvuka malengo walilojiwekea.

Amesema wamefanikiwa hayo yametokana na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato kwa kuhakikisha wanatoa elimu kwa wafanyabiashara na wajasiriamali ili kutambua umuhimu wa kulipa kodi kwa wakati.
Aidha, Mwl. Simbeye amesema kwa mwaka wa fedha 2026/27 lengo ni kukusanya zaidi ya bilioni 4.1 huku akibainisha tayari mikakati mmbalimbali imewekwa ili kuhakikisha hilo linafikiwa.
Ameongeza kuwa mapato yanayokusanywa yamekuwa yakichangia kuboresha utoaji huduma za kijamii pamoja na kuwezesha utekelezaji wa mpango wa utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, hatua inayosaidia wananchi kujiongezea kipato na kujikwamua kiuchumi.