Joy FM

Wafugaji watakiwa kuchanja mifugo yao dhidi ya ugonjwa wa sotoka Kasulu

17 September 2026, 12:30

Mifugo ikiendelea kupatiwa chanjo, Picha na Hagai Ruyagila

Chanjo ya wanyama ni muhimu sana katika ufugaji kwa sababu husaidia kuzuia magonjwa mbalimbali yanayoweza kuathiri wanyama kama ng’ombe, mbuzi, kondoo, kuku na mbwa wanaweza kushambuliwa na magonjwa ambayo yanaweza kusababisha vifo na hasara kubwa kwa wafugaji

Na Hagai Ruyagila

Wananchi na wafugaji katika Halmashauri ya Mji Kasulu Mkoani Kigoma wametakiwa kuhakikisha mifugo yao, hususan mbuzi na kondoo, inachanjwa dhidi ya ugonjwa wa sotoka kuelekea kipindi cha masika.

Wito huo umetolewa na Afisa Mifugo wa Halmashauri ya Mji Kasulu ambaye pia ni Mratibu wa Chanjo, Mariot Paul Chikwela, wakati wa zoezi la utoaji chanjo kwa mifugo katika maeneo mbalimbali ya halmashauri hiyo.

Afisa mifugo ambaye pia ni mratibu wa chanjo Halmashauri ya Mji Kasulu Mariot Chikwela, Picha na Hagai Ruyagila

Chikwela amesema halmashauri imejipanga kuendelea kudhibiti magonjwa ya mifugo yanayosababishwa na virusi kwa kutumia chanjo pamoja na kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu kinga na udhibiti wa magonjwa hayo.

Amesema chanjo hiyo inatolewa kwa ruzuku ya nusu bei, ambapo mfugaji anachanja mbuzi au kondoo mmoja kwa shilingi 300 badala ya shilingi 700, hatua inayolenga kuwawezesha wafugaji wengi zaidi kupata huduma hiyo.

Baadhi ya mifugo ikipatiwa chanjo, Picha na Hagai Ruyagila

Aidha, Chikwela amebainisha dalili za ugonjwa huo kwa mbuzi na kondoo ikiwemo mafua makali na kuharisha.

Kwa upande wao, wafugaji walioshiriki katika zoezi hilo wameishukuru Serikali kwa hatua hiyo, huku wakiomba kuendelea kupewa elimu na semina kuhusu magonjwa ya mifugo, njia za kuyazuia pamoja na namna bora ya kuyadhibiti.

Zoezi hilo limefanyika katika Kata za Kigondo, Ruhita, Nyumbigwa, Murufiti na Nyasha, kufuatia kuibuka kwa ugonjwa wa sotoka katika maeneo hayo mwishoni mwa mwezi Mei mwaka 2026.