Joy FM
Joy FM
27 August 2026, 14:25

Kutengeneza madawati huwasaidia wanafunzi kupata sehemu nzuri ya kukalia wakati wa masomo badala ya kukaa sakafuni, wanafunzi hukaa kwenye madawati na hivyo kuwa tayari kujifunza
Na Emmanuel Kamangu
Wazazi na walezi wa shule ya msingi titye kata ya titye Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu wametengeneza madawati 100 na kuyakabidhi kwa shule hiyo ili kukabiliana na wimbi la watoto kukaa chini wakati wa ujifunzaji.
Akizungumza mgeni rasmi wa hafla hiyo Bw. Respice Swetu kwa niaba ya Afisa Elimu msingi Wilaya ya Kasulu amewataka wazazi na walezi kuendelea kuwa na mtazamo chanya ili kuendelea kushirikiana na serikali katika kutekeleza shuguli za maendeleo.
Naye Afisa Elimu kata ya Titye Bw. Yoabu Hinyula amewapongeza wazazi na walezi kwa umoja wao huku akibainisha kuwa madawati hayo yatapunguza utoro kwa kiasi kikubwa.
Aidha mkuu wa shule ya msingi Titye Bw. Hilali Abudala amesema shule hiyo inakabiliwa na uhaba wa madawati 349 na kuwa kukamilika kwa madawati 100 kutafanya shule hiyo kubaki na uhaba wa madawati 249 na kuwaomba wananchi na wadau wengine wa maendeleo kuendelea kushirikiana ili kumaliza kabisa kero hiyo.

Kwa upande wao wazazi na walezi wa shule ya msingi titye wamesema wamewiwa kuchangishana fedha kwaa ajili ya kutengeneza madawati baada ya kuona watoto wao wakipitia adha kubwa ya kukaa chini wakati wa ujifunzaji na kushindwa kujifunza kwa ufanisi.
Madawati hayo 100 yamegharimu jumla ya kiasi cha Tsh million 3 na laki 1 ikiwa ni michango ambayo imetokana na jasho la wananchi ili kuhakikisha watoto wao wanasoma wakiwa katika mazingra rafiki.