Joy FM

Naibu Waziri ataka wananchi kuchangamkia mikopo ya 10% Kigoma

20 August 2026, 07:50

Muonekeano wa kiwanda cha Lukundi kinachomilikiwa na vijana ambao ni wanafaika wa mikopo ya asilimia 10, Picha na Mwandishi Wetu.

Serikali imekuwa ikitoa mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwa makundi mbalimbali, huku ikiweka msisitizo katika usimamizi na utoaji wa elimu kwa wanufaika ili kuhakikisha mikopo hiyo inaleta matokeo yaliyokusudiwa.

Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Zainab Katimba, amewataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kuendelea kutoa elimu na hamasa kwa wananchi, hususan wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, kuhusu mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri.

Bi. Zainab ametoa wito huo Agosti 18, 2026, wakati wa ziara yake ya kutembelea vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu vinavyonufaika na mikopo hiyo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Wanawake wa kikundicha Women Group kinachujihusisha na ufumaji wa mashauka baada ya kunufaika na mikopo, Picha na Mwandishi Wetu

Amesema Maafisa Maendeleo ya Jamii, kuanzia ngazi ya kata, wana wajibu wa kuwaelimisha wananchi kuhusu fursa hiyo pamoja na matumizi sahihi ya mikopo ili iweze kuchochea shughuli za kiuchumi na kuongeza kipato.

“Serikali itaendelea kutoa mikopo hiyo na kusimamia utekelezaji wake ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata fursa ya kutumia mitaji hiyo katika shughuli za uzalishaji” amesema Katimba.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Zainab Katimba, alipokuwa ametembelea kikundi cha akina mama cha Women Group, Picha na Mwandishi Wetu

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri ametembelea vikundi vitano ambavyo ni Upendo Women, kinachojihusisha na ufumaji na uuzaji wa mashuka; Unique Women, kinachofanya ufugaji wa kuku wa nyama na mayai; Azania Bakery, kinachojihusisha na uuzaji wa vitafunwa; Lukundo, kinachotengeneza kinywaji cha tangawizi; na Tito Phone Accessories, kinachojihusisha na uuzaji na utengenezaji wa vifaa vya simu.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Zainab Katimba, akiwa anaangalia shuka la kufumwa alipotembelea kikundi cha wanawake cha Women Group, Picha na Mwandishi Wetu

Wanufaika wa mikopo hiyo wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuwapatia fursa hiyo, wakieleza kuwa imewawezesha kujiajiri, kuajiri wengine, kugharamia elimu ya watoto wao na kuboresha maisha yao kiuchumi.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Zainab Katimba, akiwa amemtembelea mlemavu ambaye ni mnufaika wa mkopo wa asilimia 10, Picha na Mwandishi Wetu

Mikopo ya asilimia 10 hutolewa na Halmashauri kupitia mapato yake ya ndani kwa ajili ya kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za kiuchumi.