Joy FM

Ujenzi bandari ya Lagosa ziwa Tanganyika wafikia 96%

11 October 2023, 11:43

Waziri wa Uchukuzi akiwa katika ukaguzi wa ujenzi wa bandari ya lagosa iliyopo Wilayani Uvinza, Picha na Tryphone Odace

Hatua ya kuanza ujenzi wa Bandari ya Lagosa iliyopo Wilayani Uvinza Mkoani Kigoma inatajwa kuwa mkombozi kwa wananchi wanatumia ziwa hilo kusafirisha bidhaa zao ikiwmo Nchi jirani za Congo na Burundi.

Na Tryphone Odace

Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa, amewahakikishia wananachi  wa vijiji vya mwambao wa Ziwa Tanganyika wilayani Uvinza mkoani Kigoma, kuwa mradi wa bandari ya Lagosa inayojengwa katika kijiji cha Mgambo wilayani humo kwa gharama ya Shilingi Bilioni 15 utakamilika kwa asilimia 100% katika muda wa miezi sita ijayo.

Utekelezaji wa mradi huo ambao kwa sasa umefikia asilimia 96%, ulianza mwaka 2017 lakini ulisimama kwa sababu ya changamaoto kadhaa, ikiwemo kuongezeka kwa kina cha maji katika Ziwa Tanganyika.

Muonekano wa bandari ya Lagosa Wilayani Uvinza ambayo inaendelea kujengwa, Picha na Tryphone Odace

Hata hivyo Waziri Profesa Mbarawa ambaye amezuru katika eneo la ujenzi wa bandari hiyo amearifiwa kuwa changamoto hizo sasa zimekwisha, hivyo amewahakikishia wananchi kuwa mradi huo utakamilika katika kipindi cha miezi sita kuna kuanza kutoa huduma kwani serikali inatambua umuhimu wa mradi huo kwa wananchi wa maeneo hayo.

Naye Mkurugenzi wa Huduma za Biashara ya Meli kutoka Shirika la Uwakala wa Meli nchini TASAC, Nelson Cosmas Mlali akimwakilisha mkurugenzi mkuu shirika hilo linalosimamia na kudhibiti usafiri kwa njia ya maji, amewapongeza wadau wa usafiri huo katika maeneo hayo kwa kuzingatia sheria za vyombo vya majini na kusaidia kuepuka ajali za mara kwa mara.