Joy FM
Joy FM
21 May 2026, 12:27

Mfumo wa NEST ni mfumo wa kielektroniki unaotumiwa na serikali kusimamia zabuni mbalimbali za umma na kupitia mfumo huu, wajasiriamali wanaweza kuona matangazo ya zabuni, kutuma maombi na kufuatilia taarifa mbalimbali zinazohusu manunuzi ya serikali kwa njia ya mtandao NEST Tanzania
Na Mwandishi wetu
Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt. Rashid Chuachua amevihimiza vikundi vya wajasiriamali katika Manispaa ya Kigoma Ujiji na Wilaya ya Kigoma kwa ujumla, kuchangamkia fursa za asilimia 30 % za manunuzi ya umma kwa kujiunga katika mfumo wa NEST ili kupata zabuni zitakazowasadia kukua kiuchumi.
Amesema hayo jana wakati akifungua mafunzo ya fursa za asilimia 30% za manunuzi ya umma kwa makundi maalum ya vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu kutoka kata sita za Manispaa ya Kigoma Ujiji, yaliyolenga kuwapatia elimu juu ya mfumo wa manunuzi ya umma (NEST), ili waweze kunufaika na zabuni mbali mbali za serkalini.

Inaelezwa katika zabuni zitolewazo na serikali asilimia 30% ya zabuni hizo zimetengwa maalum kwa ajili ya vikundi vya wajasiriamali, lakini katika Manispaa ya Kigoma Ujiji ni vikundi 12 tu ndivyo vimejisajili katika mfumo wa NEST kwa ajili ya kuweza kuomba zabuni hizo kati ya vikundi 317.

Baadhi wa wanachama wa vikundi wamesema ukosefu w elimu kuhusiana na asilimia 30% za manunuzi ya umma umechangia kuwakosesha fursa hiyo na kwamba baada ya mafunzo sasa wako tayari kujiunga na mfumo huo.