Joy FM
Joy FM
22 April 2026, 12:19

Wanawake Wilayani uvinza Mkoani Kigoma wametakiwa kuchangamkia fursa zilizopo katika maeneo yao ikiwemo mikopo ya kuwawezesha kufanya shughali mbalimbali za kiuchumi ili kuwasaidia kuepukana na uchumi tegemezi
Na Mwandishi wetu
Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza imezindua rasmi jukwaa la uwezeshaji wanawake kiuchumi katika ukumbi wa Halmashauri, ikiwa ni hatua muhimu ya kukuza maendeleo na ustawi wa wanawake katika jamii.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mh. Dinah Mathamani, amesema jukwaa hilo lina lengo la kuwainua wanawake kiuchumi kwa kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali, kuongeza kipato na kujenga maisha bora kwa familia na jamii kwa ujumla.

Aidha, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Wilaya ya Uvinza, Godfrid Nkuba, amewasihi wanawake waliochaguliwa kutoka kila kata kuhakikisha wanatumia majukwaa hayo kama nyenzo ya kuhamasisha maendeleo, kubadilishana uzoefu, na kuibua fursa mbalimbali za kiuchumi zitakazowanufaisha wanawake wengi zaidi.

Uzinduzi wa jukwaa hilo unatarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko chanya kwa wanawake wa Wilaya ya Uvinza, kwa kuwapa nafasi ya kujifunza, kushirikiana na kuimarisha uwezo wao wa kiuchumi.