Joy FM

Walimu wakuu wapatiwa zana za ufundishaji na ujifunzaji Kasulu

14 May 2026, 13:11

Baadhi ya walimu wakuu ambao wamepewa zana za ufundishaji, Picha na Emmanuel Kamangu

Serikali pamoja na wadau wa elimu wameendelea kuchukua juhudi mbalimbali za kuboresha sekta ya elimu nchini Tanzania na miongoni mwa juhudi hizo ni utoaji wa zana za ufundishaji na ujifunzaji

Na Tresipholi Odace

Walimu wakuu katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu wamepatiwa zana za ufundishaji na ujifunzaji  pamoja na mafunzo maalumu kupitia program ya Memkwa iliyoko chini ya mradi wa elimisha mtoto ili kuhakikisha  wanaongeza  ufaulu mashuleni.

 Akizungumza Afisa elimu Taaluma msingi Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Bw. Michael Ngobe wakati wa mafunzo hayo  ambayo yamelenga kuwajengea uwezo walimu juu ya  namna ya  kutengeneza zana  za ufundishaji   amesema kunakila sababu za kuhakikisha walimu wote katika halmashauri hiyo wanapatiwa mbinu bora za ufundishaji lengo ikiwa  ni kuwajengea uwezo walimu wa Mpango wa Elimu Kwa Waliokosa yaani MEMKWA .

Aidha Bw Ngobe amehimiza walimu kutambua umuhimu wa kutunza takwimu ili kusaidia   kupima matokeo ya matumizi ya zana za ufundishaji kwa watoto mashuleni.

Afisa elimu Taaluma msingi Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Bw. Michael Ngobe, Picha na

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo mmoja wao akiwa  Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mvugwe Bi Marystella Ndigeza wamesema mafunzo hayo yatawasaidia kuongeza maarifa ya ufundishaji jambo litakalosaidia kuongeza ufaulu kwa wanafunzi.

Mafunzo haya yanayoendeshwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) yanalenga kuhakikisha walimu wanatambua umuhimu wa kufundisha kwa vitendo na kutumia mbinu za kisasa kufundishia ili  kuongeza ufaulu mashuleni.