Joy FM
Joy FM
4 May 2026, 16:36

Wananchi Mkoani Kigoma wamepongeza watumishi wa umma kwa kujitoa kikamilifu kuhakikisha Jamii inapata huduma bora ikiwemo elimu na afya hali ambayo imesaidia kuondoa migogoro iliyokuwa inatokana na kukosa huduma kwa wakati.
Na Hagai Ruyagila
Watumishi wa sekta ya umma na taasisi binafsi mkoani Kigoma wametakiwa kutimiza wajibu wao kwa kufanya kazi kwa uadilifu na kuzingatia muda wa kazi ili kuwahudumia wananchi kwa ufanisi katika maeneo yao ya kazi.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Simon Sirro, wakati akizungumza na watumishi wa umma na taasisi binafsi wilayani Uvinza.
Amesema kuwa mtumishi wa umma anapaswa kuweka mbele maslahi ya wananchi kwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo badala ya kujikita katika shughuli binafsi akiwa kazini, jambo litakalosaidia kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.
Aidha, Simon Sirro amewasisitiza waajiri wote wa sekta ya umma na binafsi kuzingatia sheria za kazi pamoja na kuhakikisha wafanyakazi wanapata stahiki zao kwa wakati, ili kuongeza ufanisi na ari ya utendaji kazi.
Kwa upande wake, Katibu wa TALGWU mkoa wa Kigoma, Johnson Muyombya, ameishukuru serikali kwa namna inavyoendelea kuwajali watumishi wake nchini, hali ambayo imekuwa chachu ya kuongeza morali na bidii katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.