Joy FM
Joy FM
16 July 2026, 17:18

Wazee ni nguzo muhimu katika familia na jamii. Wao ni watu waliotangulia kwa umri na wana uzoefu mkubwa wa maisha. Kwa sababu hiyo, ni wajibu wa kila mtu kuwaheshimu na kuwajali
Na Hagai Ruyagila
Shirika la Endeleza Wazee Kigoma (EWAKI) limezindua rasmi mradi wa kuimarisha sauti za wazee Wilaya ya Kasulu wenye lengo la kuibua na kutatua changamoto zinazowakabili wazee katika jamii.
Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi mkubwa wa mikutano wa Halmashauri ya Mji Kasulu, ambapo wazee wamepata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali na kupatiwa majibu papo kwa papo kutoka kwa wataalamu.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Naibu Mkurugenzi wa Shirika la Endeleza Wazee Kigoma (EWAKI), Frank Baseka amesema lengo la mradi huo ni kusikiliza na kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili wazee kwa kuimarisha ushirikiano na Serikali, asasi za kiraia, wadau mbalimbali na wataalamu kutoka Halmashauri.

Aidha, ameeleza kuwa mradi huo utaanza kutekelezwa katika kata tisa wazee watapatiwa elimu kuhusu usalama wa kipato na uchumi, afya pamoja na mapambano dhidi ya ukatili.
Afisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji Kasulu, Festo Solly amesisitiza umuhimu wa kuanzisha na kuimarisha afua zinazohusika na masuala ya wazee sambamba na kuhakikisha wazee wote wanashirikishwa kikamilifu katika maamuzi ya maendeleo ndani ya familia na jamii kwa ujumla.

Katibu wa wazee halmashauri ya Mji Kasulu Letisia Homela amelishukurushirika la EWAKI kwa kuanzisha mradi huo akieleza kuwa utawapa fursa ya kuwawezesha kiuchumi kutoa maoni, kueleza changamoto zinazowakabili na kushiriki kikamilifu katika kutafuta suluhisho litakaloboresha ustawi na maisha yao katika jamii.