Joy FM
Joy FM
17 July 2026, 13:19

Mradi wa umwagiliaji wa bonde la Mto Luiche unaotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma ni miongoni mwa miradi mikubwa ya maendeleo inayolenga kuimarisha sekta ya kilimo nchini
Na Tryphone Odace
Serikali imeanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa umwagiliaji wenye thamani ya shilingi bilioni 65 katika Bonde la Mto Luiche katika Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma, Mkoani Kigoma ukiwa na lengo la kuongeza uzalishaji zao la Mpunga ili kuimarisha usalama wa chakula na kuinua kipato cha wakulima.
Akizungumza wakati wa kukagua maendeleo ya mradi huo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro, amesema serikali imewekeza fedha hizo ili kuhakikisha wakulima wanaondokana na kilimo cha kutegemea mvua na kuingia katika kilimo cha kisasa chenye tija.
Naye Kaimu Mhandisi wa Umwagiliaji Mkoa wa Kigoma Ally Rashid amesema kazi zinaendelea na ujenzi wa barabara za kufika kwenye mto huo.

Kwa upande wake, Afisa Kilimo wa wilaya Kigoma Ramadhani Mpasuakomu amesema mradi huo utasaidia kuongeza eneo la umwagiliaji, kuboresha matumizi ya rasilimali za maji na kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara.
Baadhi ya wananchi wa Bonde la Mto Luiche wameeleza matumaini makubwa waliyonayo kuhusu mradi huo.

Mradi wa umwagiliaji wa Bonde la Mto Luiche unatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo ya sekta ya kilimo ukichangia kuongeza uzalishaji wa mazao, usalama wa chakula na kukuza uchumi wa wananchi wa Mkoa wa Kigoma.