Joy FM
Joy FM
30 April 2026, 10:23

Maadili mema ni mwongozo muhimu katika maisha ya kila siku ya mwanafunzi kwani huakisi tabia njema kama nidhamu, uaminifu, heshima, na bidii kwa mwanafunzi mwenye ndoto ya kufanikiwa maishani, maadili haya huwa nguzo kuu inayomsaidia kufikia malengo yake.
Na Hagai Ruyagila
Wanafunzi wanaotarajia kuhitimu kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Kasulu Mkoani Kigoma wametakiwa kuzingatia maadili mema, kuwaheshimu wazazi wao na kujiepusha na vitendo vya uhalifu ili kulinda mustakabali wao na kuwa raia wema katika jamii.
Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya Sekondari Kasulu Twalib Mangu wakati wa mahafali ya 16 ya kidato cha sita ambayo yamefanyika shuleni Hapo.

Amesema ni muhimu kwa wahitimu hao kutambua thamani ya elimu waliyoipata na kuitumia kwa manufaa yao binafsi na ya jamii kwa ujumla, huku akiwataka kuwa mabalozi wazuri wa nidhamu na maadili mema.
Mkuu wa Shule ya sekondari Kasulu Mwl Denis Kiloti amesisitiza umuhimu wa wanafunzi kuwaheshimu na kuwatii wazazi wao, huku akiwataka wazazi kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulea, kuwasimamia na kuwaongoza watoto katika misingi bora ya maadili.

Katibu wa Jumuiya ya Wazazi wilaya Ya Kasulu Mapigano nduhilubusa amesiwasisitiza vijana hao wanaotarajia kuhitimu kidato cha Sita kuepuka matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.

Baadhi ya wanafunzi wameeleza kufurahishwa na hatua waliyofikia huku wakiahidi kuwa waadilifu, kuitumia vyema elimu waliyoipata pamoja na kuzingatia maadili mema katika maisha yao yasasa baadaye.