Joy FM
Joy FM
19 May 2026, 10:12

Maji ni rasilimali muhimu katika maisha ya binadamu na maendeleo ya taifa lolote na binadamu hutegemea maji kwa matumizi ya nyumbani, kilimo, ufugaji, viwandani pamoja na shughuli nyingine za kiuchumi.
Na Sadiki Kibwana
Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Manispaa ya Kigoma Ujiji KUWASA imesema itaendelea kuwekeza zaidi katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya maji hasa katika maeneo korofi ili kuhakikisha upatikanaji wa maji unakuwa wa uhakika kwa wananchi.
Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Huduma kwa wateja Mamlaka ya Maji Safi na Mazingira Manispaa ya Kigoma Ujiji KUWASA Filipo Funga, wakati akizungumza na kipindi hiki ambapo amesema maboresho hayo yatajikita katika maeneo yote korofi huku shilingi bilioni 5 zikitarajiwa kutumika.
Aidha ameongeza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya maji ni muhimu na wamepanga kila mwaka kuboresha maeneo yenye miundombinu chakavu ili upatikanaji wa maji uwe wa kutosha wakati wote.
Baadhi ya wananchi wamesema mpango huo ukikamilika utakuwa na manufaa makubwa Katika upatikanaji bora wa huduma ya maji.
Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha huduma ya maji nchini kwa kujenga na kuboresha miundombinu ya maji safi na usafi wa mazingira, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo muhimu kwa urahisi na uhakika.