Joy FM

Kasulu yatenga zaidi ya milioni 200 mikopo ya 10%

24 July 2026, 14:06

Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Mji Kasulu Mwl Vumilia Julius Simbeye akiongea na vyombo vya habari kuhusu serikali kutenga zaidi ya shilingi milioni 200 ili waje kujitokeza kuomba mikopo kupitia vikundi watakavyokuwa wameviunda, Picha na Hagai Ruyagila

Mpango wa mikopo ya asilimia 10 umeendelea kuwa chachu ya maendeleo ya vikundi kwa kuongeza mtaji, kuimarisha shughuli za kiuchumi, kuongeza ajira na kipato cha wanachama, pamoja na kuboresha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

Na Hagai Ruyagila

Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma imetenga zaidi ya shilingi milioni 200 kwa robo ya kwanza ya Mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi vya wanawake, Vijana na Watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kujikwamua kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali za uzalishaji.

Akizungumza na vyombo vya habari, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji Kasulu, Mwl. Vumilia Simbeye, amesema halmashauri hiyo tayari imefungua dirisha la mikopo hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ikiwa ni utekelezaji wa maagizo  ya Serikali kwa halmashauri kutenga asilimia 10 ya fedha zinazotokana na mapato ya ndani ya halmashauri kwa ajili ya vikundi mbalimbali.

Mwl. Simbeye amesema kutengwa kwa zaidi ya shilingi milioni 200 kwa Mwaka huu wa fedha kunatoa fursa kwa wananchi wengi zaidi kunufaika na mikopo hiyo. Akisisitiza wananchi kujiunga katika vikundi vinavyotambulika na kujitokeza kuomba mikopo hiyo.

Sauti ya Mwl. Vumilia Simbeye

Aidha Mwl Simbeye amesema kwa Mwaka wa fedha uliopita 2025/2026 Halmashauri hiyo imetoa mikopo ya zaidi ya shilingi milioni 600 kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Sauti ya Mwl. Vumilia Simbeye

Mratibu wa mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na Vijana, Wanawake na Watu wenye ulemavu Halmashauri ya Mji Kasulu, Godfrey Jeremiah, amezungumzia sifa zinazotakiwa kwa waombaji wa mikopo hiyo ikiwemo kuwa na namba ya nida.

Sauti ya Godfrey Jeremiah
Mratibu wa mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na Vijana, Wanawake na Watu wenye ulemavu Halmashauri ya Mji Kasulu, Godfrey Jeremiah, Picha na Hagai Ruyagila

Baadhi ya wananchi wa Halmashauri ya Mji Kasulu wameipongeza Serikali kwa kuendelea kutenga fedha za mikopo ya asilimia 10, wakisema mpango huo umekuwa chachu ya kuanzisha na kupanua shughuli za kiuchumi, kuongeza kipato cha kaya na kuboresha ustawi wa familia zao.