Joy FM
Joy FM
23 May 2026, 13:23

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro amekagua kisha kuzungumza na wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao katika soko la Kibirizi, Manispaa ya Kigoma Ujiji, kufuatia kuungua kwa baadhi ya vibanda vya biashara visivyo vya kudumu, vilivyojengwa jirani na soko hilo.
Na Tryphone Odace
Mkuu wa Mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro ameagiza kufanyika kwa uchunguzi na kuchukuliwa hatua za kisheria kwa yeyote aliyehusika na tukio la moto uliosababisha jumla ya vibanda tisa vya biashara kuteketea kwa moto katika soko la Kibirizi Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Akizungumza na wafanyabiashara baada ya kutembelea eneo hilo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro ameagiza uchunguzi wa kina kufanyika mara moja ili kubaini aliyehusika aweze kuchukuliwa hatua na kuwaomba wafanyabiashara kuendelea na shughuli zao wakati wakisubiri sokola jipya la Kibirizi likamilike ili waweze kuhamia katika soko hilo.
Awali akitoa taarifa ya tukio hilo mbele ya Mkuu wa Mkoa Kigoma, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Kigoma Michael Maganga amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa chanzo cha moto huo jiko la mkaa liliachwa na mmoja wa wafanyabiashara akiwa ameinjika maharage katika eneo hilo.

Baadhi ya wafanyabiashara waliozungumza na Joy Fm wameiomba serikali kuwasaidia mikopo wafanyabiashara walioathirika na tukio hilo la moto ili waweze kurejea katika shughuli zao za kila siku.
Hata hivyo Mkuu wa Mkoa Kigoma, Balozi Simon Sirro ameelekeza wananchi kuendelea kushirikiana katika suala la ulinzi wa maeneo ya biashara ili kukabiliana na watu wenye nia ovu katika maeneo yao