Joy FM

Vijana wahimizwa kujitambua na kulinda amani Kigoma

13 August 2026, 14:52

Baadhi ya vijana waliohudhuria hafla hiyo ya vijana. Picha na Sadick Kibwana

Wadau wa maendeleo Manispaa ya Kigoma Ujiji wameeleza kuwa vijana hawana budi kujikita kwenye shughuli za uzalishaji mali zitakazowasaidia kujipatia kipato.

Na Sadik Kibwana

Vijana katikaa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Mkoani Kigoma, wamehimizwa kujitambua, kulinda amani ya nchi na kuwa mstari wa mbele katika shughuli za uzalishaji mali ili kujenga maisha bora na kuinua uchumi wao.

Wito huo umetolewa wakati wa maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, yaliyoandaliwa na Taasisi ya Kigoma Youth Development and Allied (KIVIDEA) Mkoani Kigoma.

Baadhi ya vijana waliohudhuria hafla hiyo ya vijana, Picha na Sadick Kibwana

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Afisa Vijana wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Bw. VenanceRichard Kasimo, amewataka vijana kutumia fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali, huku wakijiepusha na makundi rika yasiyokuwa na tija katika maendeleo yao.

Sauti ya Afisa Vijana wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Bw. VenanceRichard Kasimo
Afisa vijana Manispaa ya Kigoma Ujiji, Picha na Sadick Kibwana

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa KIVIDEA, Babu Pasco, amewataka vijana kuchukua hatua na kujikita katika shughuli za maendeleo zitakazowawezesha kujitegemea kiuchumi.

Amesema KIVIDEA itaendelea kuwawezesha vijana kupitia mafunzo ya ujasiriamali na ujuzi mbalimbali, huku akiwataka kutumia maarifa wanayopata katika kujenga maisha yao.

Sauti ya Mkurugenzi Mtendaji wa KIVIDEA, Babu Pasco

Naye Mratibu wa Taasisi ya KIVIDEA, Zabron Joseph, amesema maadhimisho hayo yamefanikisha lengo la kuwafikishia vijana elimu na uelewa kuhusu namna ya kutumia fursa zilizopo kwa ajili ya maendeleo yao.

Amesisitiza kuwa vijana wanapaswa kuchagua njia sahihi za kufikia malengo yao ili kuwa na maisha bora na familia zenye msingi imara hapo baadaye.

Sauti ya mratibu KIVIDEA
Baadhi ya viongozi waliohudhuria mkutano huo, Picha na Sadick Kibwana

Baadhi ya vijana walioshiriki katika maadhimisho hayo wamesema wamepata elimu, maarifa na hamasa ya kujitegemea kupitia shughuli mbalimbali zilizofanyika.

Sauti ya vijana

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo: “Mazingira Tofauti, Fursa Sawa kwa Vijana.”

Kaulimbiu hiyo inasisitiza umuhimu wa kuhakikisha vijana wanapata fursa sawa za kushiriki katika maendeleo, bila kujali mazingira wanayoishi au changamoto zinazowakabili.