Joy FM

Baraza la watoto Buhigwe lajadili mapambano dhidi ya ukatili

13 May 2026, 12:50

Baadhi ya wanafunzi wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Buhigwe baada ya mjadala wa baraza la watoto, Picha na Ofisi ya Buhigwe Dc

Baraza la watoto lina mchango mkubwa katika kuhakikisha watoto wanaishi katika mazingira salama, yenye upendo na heshima kwa haki zao

Na Mwandishi wetu

Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii kwa kushirikiana na World Vision, imefanya kikao cha Baraza la Watoto ngazi ya Wilaya kilichofanyika Mei 8, 2026 katika ukumbi wa Jengo la Vijana.

Katika kikao hicho, watoto walijadili madhara ya ukatili wa kijinsia kwa watoto, familia na jamii kwa ujumla. Pia walipata elimu kutoka kwa wataalamu kuhusu namna ya kukabiliana na ukatili, ukatili wa mtandaoni pamoja na afya ya uzazi na mahusiano kwa vijana.

Baadhi ya wanafunzi wakiwa kwenye baraza la watoto wilaya Buhigwe, Picha na Buhigwe DC 2013

Akisoma risala kwa mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Watoto Wilaya ya Buhigwe, Gloria Alex Gabriel, aliishukuru Serikali kupitia Maafisa Maendeleo ya Jamii na Maafisa Ustawi wa Jamii kwa kuendelea kutoa elimu ya malezi, haki na ulinzi wa watoto. Pia alilipongeza World Vision kwa mchango wake katika utekelezaji wa afua mbalimbali za watoto na jamii wilayani humo.

Kwa upande wake, mgeni rasmi Amina Kaniki, Afisa Maendeleo ya Jamii, ambaye ni Mratibu wa dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Kigoma aliwapongeza wajumbe wa baraza hilo na kuwahimiza kuendelea kutoa elimu kwa watoto wenzao katika ngazi za vijiji na kata, pamoja na kutoa taarifa mapema wanapoona viashiria vya vitendo vya ukatili.

Amina Kaniki, Afisa Maendeleo ya Jamii, ambaye ni Mratibu wa dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Kigoma, Picha na Buhigwe dc 2013

Aidha, Maafisa Maendeleo ya Jamii ngazi ya kata wametakiwa kuendelea kuyaimarisha na kuyahuisha mabaraza ya watoto kila mwaka ili kupata viongozi bora wa uwakilishi wa watoto katika vijiji, kata na wilaya.