Joy FM
Joy FM
6 May 2026, 14:18

Wananwake katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji wamwetakiwa kuchangamkia fursa za kiuchumi zinazowazunguka hasa katika kilimo na uvuvi ili waweze kujikwamua kiuchumi
Na Mwandishi wetu
Katibu Tawala wa Wilaya Mganwa Nzota amezindua rasmi jukwaa la uwezeshaji wanawake Kiuchumi ngazi ya Wilaya katika Ukumbi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji.
Jukwaa hilo lina lengo la kuwainua Wanawake kiuchumi kwa kuwapatia fursa ya kukutana na kujadili masuala mbalimbali yanayohusiana na sekta za kilimo, ufugaji, uvuvi, madini, ujenzi na uchukuzi. Pia linakusudia kuongeza ushiriki wa Wanawake katika sekta za elimu, uraia, malezi na maadili, pamoja na kuwawezesha kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, uzinduzi huo uliambatana na uchaguzi wa viongozi uliowahusisha washiriki kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji na Halmashauri ya Wilaya Kigoma.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mheshimiwa Nzota amewasisitiza wajumbe kutumia kikamilifu fursa zinazotolewa kupitia majukwaa ya uwezeshaji Wanawake kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, pamoja na utekelezaji wa malengo 17 ya Maendeleo ya Milenia ya mwaka 2000, yanayolenga kuchochea maendeleo ya haraka katika jamii.
