Joy FM
Joy FM
17 July 2026, 14:40

Biashara ni nguzo muhimu ya maendeleo ya uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla
Na Sadick Kibwana
Wafanyabiashara wanawake Mkoani Kigoma wametakiwa kutumia kikamilifu teknolojia, kurasimisha biashara zao na kuzitumia fursa za kiuchumi zinazowazunguka ili kuongeza tija na kuchangia katika maendeleo ya jamii.
Wito huo umetolewa katika mdahalo uliowakutanisha wadau wa sekta ya umma na binafsi kujadili Changamoto, Taratibu na Mageuzi ya Kanuni kwa Mazingira Wezeshi ya Biashara kwa Vijana Wanawake.” Mdahalo huo umeandaliwa na Shirika la Enabel kupitia Mradi wa Wezesha Binti ambao umefanyika mjini Kigoma.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mdahalo huo, Afisa Biashara wa Mkoa wa Kigoma, Moshi Ndimligo amesema licha ya juhudi zinazofanyika, wafanyabiashara vijana wanawake bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazokwamisha ukuaji wa biashara zao.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Chemba ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania (TWCC) Mkoa wa Kigoma, Bi. Chichi Kamandwa, amesema mdahalo huo umeandaliwa ili kuwapa wafanyabiashara vijana wanawake nafasi ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuunganishwa na wadau mbalimbali wanaoweza kuchangia ukuaji wa biashara zao.
Baadhi ya wafanyabiashara vijana wanawake walioshiriki wamesema wamepata maarifa mapya kuhusu uendeshaji wa biashara, pamoja na fursa ya kukutana na taasisi na wadau mbalimbali wanaoweza kuwasaidia kukuza biashara zao.
Aidha, Shirika la Enabel linaendelea kushirikiana na Chambe ya Wafanyabiashara Wanawake Mkoa wa Kigoma kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuwawezesha vijana na wanawake kiuchumi, ikiwemo utoaji wa mafunzo ya ujasiriamali, mitaji na ushauri wa maendeleo ya biashara.
