Joy FM
Joy FM
10 October 2025, 11:45

Katika kuhakikisha walimu wanaendelea kuwa mahiri katika ufundishaji serikali imeendelea kuwapa ujuzi wa walimu ili kufahamu namna ya kutengeneza zana za kufundishia wanafunzi.
Na Tryphone Odace
Mafunzo ya uandaaji na utengenezaji wa zana za kufundishia na kujifunzia kwa Walimu mahiri wa darasa la kwanza yaliyoanza jana Oktoba 08, 2025 katika shule ya msingi Kigoma tayari yameanza kuonyesha mafanikio.
Mafunzo hayo yanafanyika kwa Walimu wa Shule za Msingi za Manispaa ya Kigoma/Ujiji na Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma chini ya mradi wa shule bora.

Moja ya washiriki wa mafunzo hayo ni Mwalimu Jetta Ndororo na Mwalimu Metus Steven wanasema mafunzo hayo yanawajengea uwezo wa uandaaji wa zana za kufundishia na kujifunzia zinazorahisisha na kukuza viwango vya ujifunzaji wa Kusoma, kuandika na kuhesabu (KKK) kwa wanafunzi wa darasa la kwanza.
Shule bora ni programu ya elimu inayofadhiliwa na Serikali ya Uingereza chini ya Idara ya maendeleo ya kimataifa (FCDO) na inashirikiana na ofisi ya Rais TAMISEMI na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia huku ikilenga kuboresha elimu katika shule za Serikali kwa ngazi ya Elimu ya Awali na msingi nchini Tanzania.
