Mazingira FM
Mazingira FM
24 August 2026, 11:17 am

Ushirikishwaji wa viongozi wa vitongoji, mitaa, vijiji na kata utasaidia kuongeza ushiriki wa wananchi, kwa kuwa viongozi hao wanafahamu kwa karibu wananchi na kaya zilizopo katika maeneo yao.
Na Mariam Mramba
Mkuu wa Wilaya ya Bunda, Aswege Enock Kaminyoge, amewataka watumishi wa Serikali katika idara mbalimbali wilayani Bunda kushirikiana na viongozi waliochaguliwa na wananchi katika kutekeleza kampeni mbalimbali, ili kuongeza ufanisi na kuhakikisha wananchi wanafikiwa kwa wakati.
Kaminyoge ametoa agizo hilo leo wakati akizindua zoezi la kampeni ya utoaji wa chanjo ya pili ya matone kwa watoto walio chini ya miaka 10, linalotarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 27 hadi 30, 2026, wilayani Bunda.Amesema ushirikishwaji wa viongozi wa vitongoji, mitaa, vijiji na kata utasaidia kuongeza ushiriki wa wananchi, kwa kuwa viongozi hao wanafahamu kwa karibu wananchi na kaya zilizopo katika maeneo yao.

Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amewataka wananchi kuondokana na dhana potofu kuhusu chanjo hiyo, akisisitiza kuwa ni salama na haina madhara kwa watoto.Amewataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapata chanjo hiyo kwa kuzingatia umuhimu wake katika kuwalinda dhidi ya magonjwa.
Kwa upande wake, Mratibu wa zoezi hilo Tupo Kigwe amesema kampeni hiyo itaanza Agosti 27 na kukamilika Agosti 30, 2026, ambapo wataalamu wa afya watapita nyumba kwanyumba, kwenye mikusanyiko ya watu, nyumba za ibada na vituo vya afya, ili kuhakikisha watoto wote wanaohusika wanapata chanjo hiyo.