Mazingira FM
Mazingira FM
27 August 2026, 6:40 pm

Usimamizi mzuri ni msingi muhimu unaoweza kusaidia jambo lililoanzishwa kuwa endelevu kwa muda mrefu.
Na Adelinus Banenwa
Imeelezwa kuwa ili kufanikiwa katika maisha na kutimiza maono, ni muhimu kuzingatia usimamizi mzuri pamoja na uaminifu.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Maboto Microfinance na Mbunge mstaafu wa Bunda Mjini, Robert Chacha Maboto, katika hafla ya kuadhimisha mwaka mmoja wa Taasisi ya Watoto Kwanza, chini ya Mchungaji Jeremiah Motomo.
Maboto amesema usimamizi mzuri ni msingi muhimu unaoweza kusaidia jambo lililoanzishwa kuwa endelevu kwa muda mrefu, huku akisisitiza umuhimu wa uaminifu katika kufikia malengo.

Katika hafla hiyo, Maboto ambaye alikuwa mgeni rasmi ameahidi kutoa vifaa vya shule kwa wanafunzi 50 katika shule inayomilikiwa na Taasisi ya Watoto Kwanza.

Aidha, kwa kushirikiana na Diwani wa Nyasura, Magigi Samweli Kiboko, pamoja na Diwani wa Kata ya Sazira, Michael Kweka, wameahidi kutoa printer moja na kompyuta moja kwa taasisi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kusaidia kukabiliana na changamoto zinazoikabili.

Kwa upande wake, Mchungaji Jeremiah Motomoto amesema hafla hiyo imelenga kutambua mwaka mmoja tangu kuanza kwa ujenzi wa shule inayomilikiwa na Taasisi ya Watoto Kwanza.
Amesema bado kuna mipango mbalimbali inayotarajiwa kutekelezwa kupitia taasisi hiyo, ambayo inalenga kutoa mchango na kuwa msaada kwa jamii.