

4 April 2025, 5:09 pm
Katika wiki ya wazazi jumuiya hiyo imefanya kazi mbalimbali kwenye jamii ikiwemo ufanyaji wa usafi katika maeneo mbalimbali, upandaji miti, kutembelea vituo vya afya.
Na Adelinus Banenwa
Jumuiya ya wazazi chama cha mapunduzi CCM wilaya ya Bunda kimepongeza kituo cha kulea watoto wanaotoka mazingira magumu cha St. Francis kwa malezi bora wanayoyatoa kwa watoto hao
Akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya wiki ya wazazi mwenyekiti wa jumuiya ya wazazi CCM wilaya ya Bunda ndugu Leonard Magwayega amesema ni jambo la kupongezwa kuona jitihada kubwa zinazofanywa na kituo hicho kuhakikisha watoto waliopo hapo wanalelewa katika misingi bora, usafi, lishe na afya njema ambavyo kwa pamoja ndiyo kazi kubwa inayofanywa na jumuiya hiyo.
Magwayega amesema jumuiya ya wazazi inasimamia mambo matano katika kutekeleza majukumu yake ambayo ni pamoja na Elimu, Malezi, Afya, Mazingira pamoja na Maadili ambapo kwa pamoja mambo hayo wameyakuta kwa watoto wanaolelewa na kituo cha St. Francis wanayazingatia.
Lucia John Tabuse katibu wa jumuiya ya wazazi CCM wilaya ya Bunda amesema katika wiki ya wazazi jumuiya hiyo imefanya kazi mbalimbali kwenye jamii ikiwemo ufanyaji wa usafi katika maeneo mbalimbali, upandaji miti, kutembelea vituo vya afya na leo ikiwa ni kilele kwa upande wa wilaya wamefika kituo cha kulea watoto wanaotoka mazingira magumu cha mtakatifu Francis.
Lucia ameongeza kuwa mbali na shughuli zingine walizozifanya pia walibeba zawadi kwa watoto hao lengo ni kuwatia moyo walimu na wanafunzi ili kuonesha jamii bado inawathani huku akitoa rai kwa wananchi wengine kujenga tabia ya kuwatembelea mara kwa mara watoto hao.
Kwa upande wao viongozi wa kituo hicho na watoto wamewashukuru viongozi wa jumuiya hiyo kwa kufika kituoni hapo kuwasalimia pia kuwapatia zawadi huku wakihaidi kuwa miti yote waliyoipanda viongozi hao watahakikisha wanaitunza vizuri ili iweze kukua.