Mazingira FM

NBS: Taarifa sahihi ili kupata Takwimu sahihi

16 June 2022, 11:12 pm

Wananchi wanashauriwa kutoa taarifa sahihi kwenye zoezi la sensa ya watu na makazi ili kuwezesha kupata Takwimu sahihi

Hayo yamebainishwa Leo June 16, 2022 wakati wa mafunzo ya ofisi ya Taifa ya Takwimu NBS kwa wahariri wa vyombo vya habari vya kijamii Tanzania yanayofanyika Mkoani Iringa tarehe 16 – 17 June 2022

 

Akizungumza katika mafunzo hayo Bi HELLEN SIRIWA Mtaalamu wa idadi ya watu kutoka ofisi ya Taifa ya Takwimu NBS amesema upatikanaji wa Taarifa sahihi unaiwezesha serikali na Taasisi zake kujua mapungufu katika huduma muhimu za kijamii kama vile Afya , elimu na miundombinu.

 

Kwa upande wa Afya bi Hellen amesema baada ya sensa serikali itabaini ni wapi kunachangamoto ya huduma za Afya kwa kulinganisha na idadi ya watu katika eneo husika vivyo hivyo kwenye elimu na miundombinu, Na haya yatafanikiwa tu endapo wananchi watatoa taarifa sahihi kulingana na maswali watakayoulizwa siku ya sensa

 

Hata hivyo amesema kamati za sensa za Wilaya na mikoa zinao wajibu wa kuendelea kuelimisha watu juu ya umuhimu wa zoezi hili na faida za sensa kwa ngazi zao kama ni Mkoa ama Wilaya inayoweza kusaidia wananchi kuona umuhimu wa sensa kwa kutumia mikutano na vyombo vya habari Bila kutumia mifano mikubwa ya kitaifa

Pia imeshauliwa kuwa mtu yeyote atakayelala kwako usiku wa kuamkia tarehe 23 kuhakikisha unataarifa zake zote ikiwa ni pamoja na umri wake, kazi yake, elimu yake, miongoni mwa maswali mengine

Ikumbukwe kwamba zoezi la sensa ya watu na makazi itafanyika kuanzia usiku wa kuamkia tarehe 23 Agosti 2022 ambapo huku kauli mbiu ya sensa hii ikiwa ni Sensa kwa Maendeleo jiandae kuhesabiwa

by Adelinus Banenwa Iringa