Mazingira FM

Ally Hapi: Nidhamu ipewe kipaumbele kwenye zoezi la sensa.

26 July 2022, 8:17 pm

Wakufunzi wa Sensa ngazi ya mkoa wa Mara wametakiwa kwenda kusisitiza suala la nidhamu kwa makarani watakaosimamia zoezi hilo.

 

Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa mkoa wa Mara,Ally Hapi,wakati akifunga mafunzo ya siku 21 kwa wakufunzi 296 wa ngazi ya mkoa.

 

Amesema zoezi la Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 ni muhimu kwa serikali kupata takwimu sahihi hivyo ni muhimu kuzingatia suala la nidhamu.

Aidha Mkuu huyo wa mkoa amesisitiza kuwa watu 6900 watakaofanya kazi hiyo ndani ya mkoa wa Mara lazima wawe watu sahihi ili zoezi hilo lisiharibike.

Kwa upande wao baadhi ya wakufunzi hao Maria Ngaero na Erastus Shilima wamesema watakwenda kufanya kazi hiyo kadri walivyojifunza kutoka kwa wakufunzi wa kitaifa na kwamba suala la nidhamu watakwenda kulizingatia ili kupata watu sahihi watakaokwenda kufanya kazi hiyo kwenye kaya.