Mazingira FM

Mtoto mwingine wa miaka 7 ajeruhiwa na fisi kijiji cha Mumagunga Bunda

28 March 2024, 9:50 am

Misipina Silivester 7 mkazi wa kitongoji cha Arusha kijiji cha Mumagunga halmashauri ya wilaya ya Bunda ameshambuliwa na fisi akiwa anaanua udaga mwambani karibu na nyumbani kwao.

Na Adelinus Banenwa

Mtoto mwingine ajeruhiwa na fisi kijiji cha Mumagunga zikiwa ni siku sita zimepita tangu mtoto wa miaka miwili kunusurika kifo baada ya kujeruhiwa vibaya na mnyama huyo.

Misipina Silivester 7 mkazi wa kitongoji cha Arusha kijiji cha Mumagunga halmashauri ya wilaya ya Bunda ameshambuliwa na fisi akiwa anaanua udaga mwambani karibu na nyumbani kwao.

Deus Lawi Mfungo mwenyekiti wa kitongoji cha Arusha kijiji cha Mumagunga ameiambia Mazingira Fm akiwa nyumbani majira ya saa mbili usiku alipata taarifa za tukio la mtoto wa Christina Mashaka kujeruhiwa na fisi.

Mfungo amesema baada ya kupata taarifa hizo alikwenda moja kwa moja nyumbani kwao na mtoto huyo ambapo mama yake alieleza kuwa tukio lilitokea majira ya saa kumi na mbili na dakika arobain na tano jioni wakati mtoto huyo akianua udaga ndipo fisi huyo aliruka na kumjeruhi sehemu ya jicho na sehemu ya shingo.

Aidha mfungo amesema kuwa kwa maelezo ya mzazi wa mtoto na mashuhuda wamesema walikuwa watoto watatu ambapo wawili kati yao walikimbia baada ya kumuona mnyama huyo ndipo alipomshambulia aliyebaki huku akibainisha kuwa mtoto huyo kwa sasa anaendelea kupata matibabu hospitali ya Kibara.

Akizungumza na Mazingira Fm mwenyekiti wa kijiji cha Mumagunga Edina Magesa Bigambo amesema tukio la mtoto kushambuliwa na kujeruhiwa na fisi limetokea March 26, 2024 majira ya jioni na kutokana na kuwepo kwa mwendelezo wa matukio hayo kwenye kijiji leo utafanyika mkutano wa kijiji ili kujua mustakali wa usalama wa jamii jiyo hasa watoto.

Ikumbukwe ni siku sita tu tangu tukio lingine kama Hilo kutokea katika kitongoji Cha Tarime kwenye kijiji hicho hicho Cha Mumagunga mtoto wa miaka 2 na miezi 9 kunusurika kifo baada ya kujeruhiwa na fisi wakati akurudi nyumbani kutoka kucheza.