Mazingira FM

WWF wafatilia kile walichowafundisha wakulima juu ya kilimo bora

27 September 2023, 11:11 pm

Wataalamu WWF wakipewa maelekezo. Picha Na Thomas Masalu

Je, mbinu iliyotolewa na WWF kuhifadhi mazingira kwa kufanya kilimo na ufugaji bora inatekelezwa?

Na Thomas Masalu

Mara ni Moja ya mikoa ya Tanzania zinazotegemea kilimo kama chanzo cha mapato na chakula kwa wananchi wake.

Hata hivyo sekta hii muhimu inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo wakulima wengi kukosa elimu sahihi ya mbinu bora za kilimo, matumizi mabaya ya ardhi na rasilimali za ardhi na changamoto za kiuchumi na biashara.

Shirika la WWF kwa kulitambua hilo liliendesha mafunzo maalumu kwa wakulima kutoka wilaya za mkoa wa Mara, mafunzo ambayo yalijikita katika kujifunza mbinu za kilimo bora kitakachosaidia pia kutuzaji Mazingira pamoja na vyanzo vya maji.

WWF kilimo bora wanachokihitaji zaidi ni kile cha kuzingatia matumizi sahihi rasilimali za kilimo na mbinu bora za kilimo ili kuhakikisha wakulima wanatumia mbinu bora za kilimo kulingana na aina ya udongo, hali ya hewa na Mazingira ili kupata mazao bora zaidi na kwa wingi.

Leo 27 Sept 2023, WWF imewatembelea wakulima wale walionufaika na mafunzo hayo ili kujionea hatua waliofikia tangu watoke kwenye mafunzo.

Sister Cecilia akizungumza na Mazingira Fm. Picha na Thomas Masalu

Sister Maria Cecilia Kasanda, wa Baraki sisters Farm wilaya ya Rorya ni mmoja wa wakulima ambao wametembelewa na WWF.

Sr, Maria amesema hadi sasa ameandaa shamba la hekari 8 kwajili ya kulima kilimo bora kinachozingatia mbinu zote walizofundishwa na WWF katika kutunzaji Mazingira.

Sr Cecilia amesema anatarajia kulima kilimo mseto ( mahindi, maharage na miti) katika shamba hilo huku akizingatia mbinu zote za kilimo bora.

Sr Cecilia amesema amechagua eneo linalofaa na ameliandaa mapema na ameandaa kutumia mbegu bora( za kisasa) zinazostahimili magonjwa na ukame.

Pamoja na hayo Sr Cecilia amesema hadi sasa ana wanafunzi wakulima 9 ambao amefundisha mbinu hizo ambapo 5 kutoka Baraki sisters Farm na watu 4 kutoka katika kijiji cha Baraki wilaya ya Rorya.

Katika hatua nyingine Sr Cecilia ameshukuru WWF kwa mafunzo waliyoyatoa kwa wakulima kwani yamekuwa chachu katika shughuli za kilimo wanazozifanya.

Sauti ya Sister Cecilia

WWF haikuishia kumtembelea sister Cecilia pekee, bali ilipiga hodi kwa Mwenyekiti wa watumia maji Nyasururi, ndugu Thomas Aron mkazi wa Kijiji cha Utegi kata ya Koryo ambaye pia ni mnufaika wa mafunzo hayo.

Mzee Aron ni mfugaji wa samaki kwa njia ya mabwawa ambapo pia naye alipata mafunzo kupitia WWF namna bora ya ufugaji samaki utakamwezesha kujipatia kipato huku akitunza Mazingira na vyanzo vya maji.

Mradi wa ufugaji samaki kwa njia ya mabwawa wa mzee Aron unajumla ya gharama milion sita na laki tatu ambapo ana jumla ya samaki elfu tatu ndani ya mabwawa.

Mradi wa ufugaji wa samaki kwa njia ya mabwawa wa mzee Aron. Picha na Thomas Masalu

Akizungumza na Redio Mazingira Fm, kwa niaba ya mzee Thomas Aron, bi Merisiana Thomas amesema wanawashukuru WWF kwa kuwapatia mafunzo ambayo wameanza kuona matunda yake.

Sauti ya Merisiana Thomas