Mazingira FM

RC Mara atoa siku 14 halmashauri Bunda Mji, Bunda wilaya kugawanya mali, madeni

24 June 2023, 8:50 am

Mkuu wa mkoa wa Mara Mhe Said Mtanda ametoa siku kumi na nne (14) kwa halmashauri ya mji wa Bunda na halmashauri ya wilaya Bunda kufanya mgawanyo wa mali na madeni ili kuondoa mkanganyiko uliopo kwa sasa.

Hayo ameyasema katika baraza maalum la madiwani la halmashauri ya Mji wa Bunda lililokaa kujadili taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali CAG hoja za mwaka 2021 na 2022 ambapo kwa halmashauri ya mji wa Bunda ilikuwa na hoja 35 ambapo kati ya hizo hoja 12 zimefungwa huku hoja 23 zikiwa katika hatua mbalimbali za utekelezaji.

Mhe Mtanda amesema anawaelekeza wakurugenzi wa halmashauri zote mbili Bunda mji na Bunda wilaya kukaa na kufanya mchanganuo wa mali na madeni huku akimtaka katibu tawala wa mkoa kusimamia zoezi hilo ndani ya siku 14 liwe limekamilika.

Aidha amemtaka mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Bunda kutengeneza gari mali ya halmashauri hiyo lililotelekezwa kwa kipindi cha mwaka mmoja ili litumike kufanya kazi za halmashauri ambapo awali mpango wa halmashauri ilikuwa kuliuza.

Aidha ameipongeza halmashauri ya mji wa Bunda kwa kupata hati safi mfululizo pia kwa kufikia asilimia 92 ya makusanyo huku akisema anaamini watavuka malengo katika makusanyo hayo.