Mazingira FM

Kambarage Wasira ashiriki kutatua changamoto shule ya msingi Kunzugu

30 September 2023, 1:50 pm

Kambarage Wasira akizungumza katika mahafali ya darasa la Saba shule ya msingi Kunzugu. Picha na Edward Lucas

Ukosefu wa choo cha walimu na vifaa vya kuchapisha mitihani ni miongoni mwa changamoto katika shule ya msingi Kunzugu iliyopo Bunda Mkoani Mara.

Na Edward Lucas

Katika mahafali ya 42 shule ya msingi Kunzugu, Kambarage Wasira ametoa ahadi ya kuwapatia ‘printa’ yenye thamani ya shilingi milioni moja na laki mbili (Tsh 1,200,000/=) kwa ajili ya kuwarahisishia huduma za uchapishaji wa mitihani na masuala mengine ya kitaaluma.

Ametoa ahadi hiyo akiwa mgeni rasmi katika mahafali hayo baada ya kupokea taarifa ya shule iliyoanisha changamoto mbalimbali zinazoikabiri shule ikiwa ni pamoja na kukosekana huduma ya ‘printa’ na ‘kompyuta’ kwa ajili ya uchapishaji wa mitihani na nakala zingine

Sauti ya Kambarage Wasira
Mwalimu Mkuu shule ya msingi Kunzugu, Yona K. Mgeniwetu akisoma taarifa ya shule katika mahafali ya 42 . Picha na Edward Lucas

Awali akisoma taarifa ya shule mbele ya mgeni rasmi na wageni wengine waalikwa, Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Yona K. Mgeniwetu amesema sambamba na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika shule hiyo kongwe iliyoanzishwa mwaka 1975 bado inakabiriwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa choo cha walimu, upungufu wa madawati na mambo mengine.

Sauti ya Mwalimu Yona Mgeniwetu
Pasaka Samson, Diwani Kata ya Kunzugu akizungumza katika mahafali ya 42 shule ya msingi Kunzugu. Picha na Edward Lucas

Naye Diwani wa Kata ya Kunzugu, Pasaka Samsoni ameahidi kuendelea shughulikia changamoto zinazoikabiri shule hiyo huku akiwapongeza wadau mbalimbali waliojitoa katika kutatua baadhi ya changamoto katika shule ya msingi Kunzugu.

Pasaka Samson, Diwani wa Kunzugu

Shule ya Msingi Kunzugu imeanzishwa mwaka 1975 mahafali ya kwanza yalifanyika mwaka 1981 ambapo kwasasa shule ina jumla ya wanafunzi 849 wavulana wakiwa 418 na wasichana 431 ikiwa na jumla ya walimu 13 kati yao wakiume ni 7 na wakike ni 6

Kwa mujibu wa taarifa ya shule wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani wa kuhitimu darasa la Saba mwaka huu 2023 jumla ni 99 kati yao wavulana ni 42 na wasichana ni 57