Mazingira FM

Changamoto ugawaji vyandarua Saranga watua kwenye kikao cha mtaa

19 August 2026, 6:22 pm

Kikao cha viongozi wa mtaa wa Saranga kata ya Kabarimu pamoja na wakazi wa mtaa wa Saranga

Miongoni mwa kero zilizowasilishwa ni zoezi la ugawaji wa vyandarua vilivyotolewa na Serikali.

Na Juma Hangi

Wakazi wa Mtaa wa Saranga wamewasilisha kero mbalimbali zinazowakabili katika kikao kilichofanyika Agosti 18, 2026, kilichoitishwa na Mwenyekiti wa Mtaa huo, Philipo Safari, kwa lengo la kujadili changamoto za wananchi na kutafuta ufumbuzi. Kikao hicho kilihudhuriwa na Diwani wa Kata ya   Kabarimu, Kulwa Ramadhan Ngata, pamoja na Mtendaji wa Kata hiyo, ambapo wananchi walipata fursa ya kueleza kero zao moja kwa moja kwa viongozi.

Miongoni mwa kero zilizowasilishwa ni zoezi la ugawaji wa vyandarua vilivyotolewa na Serikali, ambapo wananchi wamedai kuwa zoezi hilo halikufanyika kwa usawa na haki. Baadhi yao wamedai kuwa kulikuwa na utofauti wa idadi ya vyandarua walivyopatiwa wananchi, huku wakitaka viongozi kufuatilia utaratibu uliotumika katika ugawaji huo na kuhakikisha wananchi wote wenye uhitaji wanapata huduma hiyo kwa usawa.

Baadhi ya wakazi wa Saranga kwenye kikao
Baadhi ya wananchi

 Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa wa Saranga Philipo Safari  amesema kuwa madai ya ugawaji vyandarua usiokuwa na haki na usawa wameipokea ofisini na wataifanyia kazi.

Philipo Safari

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kabarimu, Kulwa Ramadhan Ngata, amesema amelichukua suala la ugawaji wa vyandarua na analifanyia kazi, huku akichukua orodha ya majina ya wananchi  ambao hawajapata vyandarua ili kufuatilia suala hilo. Aidha, amewataka wananchi wenye migogoro ya ardhi kusubiri majibu ya hatua zinazochukuliwa, ambayo amesema yatatolewa Ijumaa, Agosti 21, 2026.

Kulwa Ramadhan Ngata