Mazingira FM

Zaidi ya kilo milion 6.9 za pamba zanunuliwa Bunda

10 August 2023, 11:03 am

Mkaguzi wa zao la pamba wilayani Bunda Ndugu Hemed kabea, Picha na Adelinus Banenwa

Pamoja na idadi hiyo ya tani za pamba ambazo zimeishanunuliwa kutoka kwa wakulima hadi wakati huu kuonekana ni ndogo lakini bado wakulima wanaendelea kuuza pamba yao katika vituo vya AMCOS hivyo  kufanya mwaka huu kupiga hatua kubwa kulinganisha na miaka mingine iliyopita.

Na Adelinus Banenwa

Zaidi ya kilo milioni sita na  laki tisa za pamba sawa tani elfu  sita tayari zimenunuliwa Wilayani  Bunda, kati ya tani elfu 20 zilizokuwa kwenye malengo katika msimu wa mwaka 2022 / 2023

Hayo yamesemwa na mkaguzi wa zao la pamba wilayani Bunda Ndugu Hemed kabea wakati akitoa taarifa ya zao la pamba wilayani Bunda katika kikao kilichowakutanisha maafisa kilimo kutoka Halmashauri zote za Wilaya ya Bunda kikimjumuisha Balozi wa Pamba Nchini Mhe Aggrey Mwanri

Hemedi amesema pamoja na idadi hiyo ya tani za pamba ambazo zimeishanunuliwa kutoka kwa wakulima hadi wakati huu kuonekana ni ndogo lakini bado wakulima wanaendelea kuuza pamba yao katika vituo vya AMCOS hivyo  kufanya mwaka huu kupiga hatua kubwa kulinganisha na miaka mingine iliyopita.

Hemedi amesema kuwa katika msimu wa 2020/ 2021 Bunda ilizalisha pamba tani elfu 4.520 mwaka 2021/2022  Bunda ilizalisha tani elfu 4.546.

Balozi wa pamba Nchini Tanzania Aggrey Mwanri, Picha na Adelinus Banenwa

Kwa upande wake balozi wa pamba Nchini Tanzania Aggrey Mwanri amesema katika kuhakikisha zao la pamba linaendelea kufanya vizuri amesema bodi ya pamba imekuja na mpango wa uanzishwaji wa mashamba darasa ambayo yatakuwa chachu kwa wakulima ambapo kwa kila kitongoji kitakuwa na shamba darasa moja la mfano.

katibu tawala Wilaya ya Bunda Mhe Salumu Halfani Mtelela Picha na Adelinus Banenwa

Awali akifungua kikao hicho kwa niaba ya mkuu wa Wilaya ya Bunda,  katibu tawala Wilaya ya Bunda Mhe Salumu Halfani Mtelela amesema serikali wilayani Bunda inaunga mkono jitihada zote zinazofanywa na bodi ya pamba kwa lengo la kuinua sekta ya pamba wilayani Bunda na ameelekeza watendaji wote Wilaya ya Bunda ngazi za vitongoji , vijiji na mitaa kufanyia kazi maelekezo wanayopewa