

6 May 2025, 3:13 pm
Kutumia mbinu ya ulinzi shirikishi na kutoa elimu ili kuwafanya wananchi wawe walinzi wa maeneo hayo.
Na Adelinus Banenwa
Mkuu wa mkoa wa Mara Kanal Evance Mtambi amezitaka mamlaka za uhifadhi ikiwemo mamlaka ya hifadhi ya taifa ya Serengeti na TAWA kuimarisha mahusiano na jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi.
Maelekezo hayo ameyatoa leo tarehe 5 May 2025 katika maadhimisho ya siku ya urithi wa dunia ambayo yatafanyika Eneo la Mugumu wilaya Serengeti mkoani Mara.
Kanal Mtambi amesisitiza kutumia mbinu ya ulinzi shirikishi na kutoa elimu ili kuwafanya wananchi wawe walinzi wa maeneo hayo.
Aidha Kanal Mtambi ametoa rai kwa wananchi wanaopakana na hifadhi kwa pamoja kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa maliasili hii ambayo imerithiwa kutoka enzi za mababu.
Wakati huohuo ametoa onyo kali kwa wananchi watakaokaidi watakaokiuka na kuharibu hifadhi hizo kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa.
Kamishna msaidizi Stephano Msumi ambaye ni mkuu wa hifadhi ya taifa ya Serengeti amesema maadhimisho hayo yamefanyika Serengeti si kwa bahati mbaya bali ni kutokana na kazi nzuri inayofanyika ambapo wananchi wanashirikishwa katika shughuli mbalimbali za uhifadhi.
Maadhimisho hayo yameambatana na maonesho mbalimbali ya maeneo ya urithi wa dunia yakitanguliwa na maandamano ya amani yaliyohusisha wahifadhi pamoja na wananchi.