Mazingira FM

Mara: Viongozi wa dini,Vyama vya Siasa,Wazee wa mila na waandishi wa habari watakiwa kuunganisha nguvu kuelekea Sensa

18 August 2022, 6:06 am

Viongozi wa dini,Vyama vya Siasa,Wazee wa mila na waandishi wa habari wameombwa kuunganisha nguvu na taasisi za Serikali kuhamasisha masuala ya Sensa ili watu wote waweze kujitokeza kuhesabiwa.

Akitoa hamasa kwa makundi hayo Mkuu wa Mkoa wa Mara Meja Jenerali Suleimani Mzee leo jumanne agosti 16 katika Ukumbi wa Uwekezaji Musoma amesema,kila kundi likiwajibika katika nafasi yake zoezi hilo litafanikiwa kwa asilimia mia moja.


“Natambua umuhimu wa kila kundi hapa,na kwa kuwa suala la sensa linahusu maendeleo ya nchi yetu,naomba kila mmoja wetu kwenye eneo lake atumie siku zilizobaki kuelimisha watu hasa wale ambao hawajaelewa nia nje ya zoezi lenyewe,”amesema.


Amewataka waandishi wa habari kujikita zaidi kuandika habari za Sensa,
“tumieni Redio zenu za ndani ya mkoa,kitaifa,mitandao ya kijamii ili watu wapate uelewa ili agosti 23 washiriki vema na kuwapa ushirikiano wa kujibu vema maswali ya makarani wa sensa,”amesema.

Akizungumza kwa niaba ya waandishi wa habari Augustine Mgendi amesema,”sisi tuliofika hapa tutajitahidi lkuwashirikisha wale ambao hawajaja lengo likiwa ni kufanikisha zoezi zima la Sensa mkoa wa Mara”amesema.