Mazingira FM
Mazingira FM
25 July 2026, 9:48 pm

Wanawake wengi wanaofanya kazi migodini wanajihusisha na shughuli halali za kujipatia kipato, kinyume na mtazamo wa baadhi ya watu.
Na Edward Lucas
Uwezeshaji wa wanawake kupitia shughuli za uchimbaji madini umetajwa kuwa miongoni mwa njia zinazowasaidia kujikwamua kiuchumi na kuongeza ushiriki wao katika kugharamia mahitaji ya familia.
Hali hiyo imejidhihirisha kwa Monica Filimoni wa Mgodi wa Walwa uliopo Kinyambwiga, Wilaya ya Bunda, ambaye ametoka kuwa mama lishe hadi kumiliki mashine za kuchakata madini, maduara ya uchimbaji na mwalo wa kukamatia madini.
Monica anasema hatua hiyo ilimpa ujasiri wa kuendelea kuwekeza katika shughuli za uchimbaji, jambo lililomwezesha kupanua shughuli zake na kumiliki vifaa pamoja na maeneo yake ya uzalishaji.

Anasema mafanikio hayo yameongeza uwezo wake wa kuchangia mahitaji ya familia na kumpunguzia utegemezi wa kifedha aliokuwa nao awali.
Makamu Mwenyekiti wa Wachimbaji wa Madini Wilaya ya Bunda, Malack Silas, amesema mafanikio ya wanawake kama Monica yanadhihirisha kuwa wanawake wengi wanaofanya kazi migodini wanajihusisha na shughuli halali za kujipatia kipato, kinyume na mtazamo wa baadhi ya watu wanaodhani kuwa uwepo wao migodini unahusishwa na ukahaba pekee
Kwa mujibu wa uongozi wa mgodi wa Walwa, wanawake wameendelea kushiriki katika shughuli mbalimbali za uchimbaji na uchakataji wa madini huku mgodi ukiweka sheria na taratibu za kulinda usalama wa wachimbaji wote.
Wadau wa maendeleo wanasema kuwa kuwawezesha wanawake kiuchumi ni miongoni mwa hatua zinazoweza kuongeza ustawi wa familia na kupunguza mazingira yanayoweza kuchangia ukatili wa kijinsia.