Mazingira FM
Mazingira FM
21 August 2026, 10:18 am

Vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika maendeleo ya sekta ya pamba iwapo vitatumika vizuri na kutoa taarifa sahihi kwa wakulima na wadau wengine
Na Angel Mbalamwezi
Bodi ya Pamba Tanzania kwa kushirikiana na STV Online imetoa mafunzo kwa waandishi wa habari kutoka mikoa mitano kwa lengo la kuwajengea uelewa zaidi kuhusu uandishi wa habari zinazohusu zao la pamba.
Mafunzo hayo yamefanyika mjini Shinyanga na kuwahusisha waandishi kutoka Mara, Simiyu, Mwanza, Shinyanga na Geita.
Akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Pamba Kanda ya Ziwa Magharibi, Afisa wa Bodi ya Pamba, Penina Range, amewataka waandishi kuandika habari zenye ukweli, zilizofanyiwa utafiti na kutumia takwimu sahihi.
Amesema vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika maendeleo ya sekta ya pamba iwapo vitatumika vizuri na kutoa taarifa sahihi kwa wakulima na wadau wengine

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa STV, Sitta Tuma, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo waandishi, hususan wanaotoka katika mikoa inayolima pamba.

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Pamba nchini, Costantine Mathiasi, amesisitiza umuhimu wa waandishi kufuata kalenda ya Bodi ya Pamba ili waweze kuelewa hatua mbalimbali za zao hilo kuanzia uzalishaji hadi kufikishwa viwandani.
Naye Mwamasishaji wa maendeleo ya zao la pamba na Afisa kilimo kutoka bodi ya pamba Tz Edward nyawile amesema serikai kupitia bodi ya pamba inakuja na mikakati ya kongani na viwanda katika kuongeza uzalishaji wenye tija ikiwa ni pamoja na usanifu wa ubora wa pamba.