Mazingira FM
Mazingira FM
15 June 2026, 10:00 pm

Mollel ametoa wito huo leo wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani Bunda yenye lengo la kukagua uhai wa jumuiya, mali na miradi ya UVCCM pamoja na ujumbe wa Kuvunja makundi ndani ya jumuiya hiyo.
Na Adelinus Banenwa
Katibu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Mara, Irene Mollel, amewataka vijana wa jumuiya hiyo katika Wilaya ya Bunda kuvunja makundi yote yaliyojitokeza wakati wa uchaguzi wa mwaka 2025 na badala yake kujikita katika kukijenga chama.
Mollel ametoa wito huo leo wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani Bunda yenye lengo la kukagua uhai wa jumuiya, mali na miradi ya UVCCM pamoja na ujumbe wa Kuvunja makundi ndani ya jumuiya hiyo.

Akizungumza na viongozi na wa UVCCM wilaya ya Bunda, Mollel amewatahadharisha vijana dhidi ya kuanzisha makundi mapya au kujenga safu za uchaguzi kuelekea uchaguzi wa ndani ya chama unaotarajiwa kufanyika mwaka 2027.
Amesema nguvu za vijana zinapaswa kuelekezwa katika kuimarisha chama, kutekeleza majukumu ya kisiasa na kuendeleza miradi ya maendeleo badala ya kujihusisha na siasa za makundi ambazo zinaweza kudhoofisha mshikamano wa chama.
Katika ziara hiyo, Mollel pia alikagua ujenzi wa nyumba ya Katibu wa UVCCM Wilaya ya Bunda. Baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, amemuelekeza Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Bunda kuhakikisha ujenzi wa nyumba hiyo unakamilika kabla ya uchaguzi wa ndani ya chama unaotarajiwa kufanyika mwaka 2027.

Aidha, amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini Mhe Esther Bulaya kwa kuendelea kujitoa kwa ajili ya kukijenga Chama Cha Mapinduzi, kuziimarisha jumuiya zake pamoja na kuchochea maendeleo ya vijana ndani ya jimbo hilo. Amesema mchango wa mbunge huyo umeendelea kuleta matokeo chanya katika kuimarisha shughuli za chama na kuwapa vijana fursa za kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo.

Awali mwenyekiti wa UVCCM wilaya ya Bunda Mohamed Juma Msafiri amemuhakikishia katibu wa chama hicho kuendelea kutekeleza majukumu yao ikiwemo kutekeleza maelekezo yanayotolewa na viongozi wote ngazi za juu pia suala la uanzishwaji wa miradi ya jumuiya ili iendelee kujitegemea