Mazingira FM

Bunda DDH yaadhimisha Siku ya Wauguzi kwa harambee

15 May 2026, 1:19 pm

Pichani ni mgeni rasmi Wilson Mkama mwenye suti, katikati ni muuguzi hospitali ya Bunda DDH aliyekuwa kama Florence Nightingale, na kushoto ni Dr Andrew mganga mfawidhi Bunda DDH

Mkama alieleza kuwa anatambua kazi ya ukunga na uuguzi ni wito wa kujitolea unaoendelea kuwa msaada mkubwa kwa jamii, huku akipongeza ufanisi mkubwa wa kazi hiyo kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia duniani.

Na Adelinus Banenwa

Hospitali ya Wilaya ya Teule ya Bunda (Bunda DDH) imefanya maadhimisho ya Siku ya Wauguzi na Wakunga Duniani tarehe 15 Mei 2026, huku mgeni rasmi Ndugu Wilson Mkama akichangia shilingi milioni nane kwa ajili ya kuboresha huduma za afya hospitalini hapo.

Mchango huo umetolewa wakati wa harambee maalum iliyolenga kutatua changamoto za uhaba wa vifaa tiba kwa watoto njiti na mifumo ya hewa ya oksijeni.

Katika kilele cha maadhimisho hayo yaliyofanyika hospitalini hapo, wataalamu wa afya wametakiwa kuendeleza moyo wa kujitolea na upendo katika kuhudumia wagonjwa, hasa wakizingatia misingi iliyoachwa na mwanzilishi wa uuguzi duniani, Florence Nightingale, katika karne ya 19.

Ndugu Wilson Mkama mgeni rasmi maadhimisho ya siku ya wauguzi hospitali ya Bunda DDH

Akizungumza na wahudumu hao, mgeni rasmi Ndugu Mkama alieleza kuwa anatambua kazi ya ukunga na uuguzi ni wito wa kujitolea unaoendelea kuwa msaada mkubwa kwa jamii, huku akipongeza ufanisi mkubwa wa kazi hiyo kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia duniani.

Sauti ya Wilson Mkama
Katibu wa Hospitali ya Bunda DDH, Adelad Mchuruza,

Awali, akisoma risala mbele ya mgeni rasmi, Katibu wa Hospitali ya Bunda DDH, Adelad Mchuruza, amebainisha mafanikio makubwa ya hospitali hiyo katika utoaji wa huduma na kueleza kuwa hospitali hiyo inapokea zaidi ya watoto 300 wanaozaliwa kabla ya kufikisha miezi tisa (Watoto njiti) kila mwaka, ambapo zaidi ya watoto 120  kati yao wanatoka nje ya Halmashauri ya Mji wa Bunda.

Ili kuendelea kuokoa maisha ya watoto hao na kuboresha utoaji huduma, Katibu huyo alitoa wito kwa serikali, wadau, na taasisi mbalimbali kujitokeza kuchangia vifaa tiba zaidi. Alisisitiza kuwa hospitali inakabiliwa na uhaba wa mashine za kulelea watoto njiti na inahitaji haraka kusimikwa kwa mfumo wa kisasa wa kusambaza hewa ya oksijeni wodini badala ya kutumia mitungi ya sasa inayoleta usumbufu katika kuhudumia wagonjwa wengi kwa wakati mmoja.

Sauti ya Katibu wa Hospitali ya Bunda DDH, Adelad Mchuruza