Mazingira FM

RC HAPI AIPONGEZA HALMASHAURI YA MJI WA BUNDA KWA KUPATA HATI SAFI YA CAG KWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021

15 July 2022, 12:34 pm

Hayo yameelezwa wakati wa Baraza Maalumu la Halmashauri la kupitia Hoja za Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) tarehe 14.07.2022.

Mkuu wa Mkoa wa Mara Mheshimiwa Ally S. Hapi amewapongeza Waheshimiwa Madiwani na Wataalamu kwa kusimamia vizuri Miradi inayoletwa na Serikali katika Halmashauri ya Mji wa Bunda, Huku wakishirikiana vizuri bila migogoro ya aina yoyote.

Aidha Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa ameipongeza timu ya Wataalamu ikiongozwa na Mkurugenzi Emmanuel J. Mkongo kwa kusimamia vizuri zoezi la ukusanyaji Mapato ya Halmashauri ambapo Hadi sasa Halmashauri imefikia asilimia 105 ya Mapato kwa Mwaka wa fedha 2021/2022.

Hata Hivyo Mheshimiwa Hapi, ameielekeza Halmashauri kuongeza Nguvu zaidi katika kukusanya Mapato uku wakidhibiti matumizi kwa kuhakikisha fedha inayobaki Halmashauri inaelekezwa katika Miradi ya Maendeleo kwa Wananchi.

Katika sura nyingine, Mkuu wa Mkoa amesisitiza uwajibikaji kwa Watendaji wote wa Serikali katika Idara zao, na kuwataka kufuatilia kwa ukaribu Miradi inayotekelezwa katika maeneo yao.

Mwisho ameitaka Halmashauri kuhakikisha wanafuta Hoja zote zilizobainishwa na Mkaguzi Mkuu wa Serikali.

Kwa upande wake Mheshimiwa Joshua Nassari Mkuu wa Wilaya ya Bunda amemweleza Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa kwamba Halmashauri ya Mji wa Bunda inafanya kazi vizuri sana kwa ushirikiano baina ya Waheshimiwa Madiwani na Watumishi na ndio maana imefanikiwa kupata Hati safi ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bunda Mhe. Michael Kweka amemtoa hofu Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Mara juu ya Miradi yote inayoletwa katika Halmashauri ya Mji wa Bunda kwani yote inatekelezwa kwa Wakati na kiwango kinachostahili na kuongeza kuwa kama Kuna Miradi mingine basi asisite kuileta Halmashauri ya Mji wa Bunda.

Awali Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Bunda Ndg. Emmanuel J. Mkongo aliwasilisha kwa ufupi taarifa ya CAG kwa Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa kwa majadiliano zaidi.

Mwisho Viongozi mbalimbali walitoa salamu akiwemo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Bunda na Mheshimiwa Robert Maboto Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini.