Mazingira FM

Zitto: Bei ya pamba iendane na gharama za uzalishaji

9 June 2023, 7:43 am

Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe

Kufuatia kilio cha wakulima wa zao la pamba nchini hususani katika bei ya pamba, chama cha ACT-Wazalendo kimewaelekeza wachambuzi wake kuangalia iwapo bei hiyo inaweza kusaidia mkulima kurejesha gharama zake alizozitumia katika kilimo.

Hayo yamebainishwa na kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe wakati akifanya mahojiano na Radio Mazingira Fm Juni 8, 2023 kupitia kipindi cha Safari Mseto katika hatua za maandalizi ya chama hicho kuelekea katika mkutano wake wa hadhara uwanja wa shule ya msingi Mkendo mjini Musoma.

Zitto amesema kwa msimu uliopita bei ya pamba ilifika shilingi elfu mbili (2000) lakini katika msimu huu bei elekezi ni shilingi 1060 hivyo imepelekea malalamiko ya wakulima katika maeneo mbalimbali nchini.

“Jana tulipokuwa Busega mkoani Simiyu tulitoa mapendekezo na la rahaka ni kuhakikisha bodi ya pamba na wizara ya kilimo wafanyie kazi suala la tija kwa sababu wakulima wetu wanazalisha pamba chache sana katika kila hekari moja inayolomwa” amesema Zitto.

Zitto amesema wameishauri bodi ya pamba na wizara ya kilimo kuangalia suala la kilimo cha tija kwa kupata mazao mengi katika hekari moja na kuongeza thamani ya pamba kwa kuuza bidhaa zitokanazo na pamba mfano vitambaa.

Aidha ameishauri serikali kuwa na fao la bei kwa wakulima (Price Stabilisation) pale ambapo bei inapokuwa imeporomoka kwenye soko la dunia kiasi cha mkulima kushindwa kurejesha gharama zake, mfuko wa hifadhi za jamii umlipe ile hasara.

Zitto Kabwe yuko mkoani Mara katika mwendelezo wa uzinduzi wa mikutano ya hadhara walioanza tangu lilipoondolewa katazo la mikutano hiyo ni huu ukiwa ni mkoa wa 16 tangu waanze ziara hiyo mwezi Februari 2023.