Mazingira FM

Bunda: Vifo vya kusikitisha watoto wawili wa familia moja, msichana wa miaka 18 ashukiwa kuhusika

17 July 2023, 11:30 pm

Shimo la Choo alimokutwa mtoto Evans Martin (2). Picha na Edward Lucas

Watoto wawili wa familia moja wamefariki dunia katika matukio tofauti huku mwingine wa miaka miwili akinusurika kifo baada ya kuopolewa kwenye shimo la choo, msichana wa miaka 18 ambaye ana muda wa takribani miezi miwili tangu afike kwenye hiyo familia ashukiwa kuhusika

Na Edward Lucas

Watoto wawili wa familia moja wamefariki dunia katika matukio tofauti huku mmoja akinusurika kifo baada ya kutumbukia kwenye shimo la choo mtaa wa Nyamatoke kata ya Mcharo Wilaya ya Bunda Mkoani Mara.

Tukio la kwanza lilitokea tarehe 5 July 2023 majira ya saa 11 jioni mtoto Evalin Martin(10) alikufa maji kwa kutumbukia kwenye mkondo wa mto Rubana wakati alipokwenda kuchota maji wakiwa wameambatana na msichana aliyetambulika kwa jina la Helena ambaye ni mtoto wa shangazi yake.

Akisimulia tukio hilo Neema Maduhu Gedi (47) ambaye ni mama wa Evalin amesema masaa machache baada ya mwanaye kuelekea mtoni akiwa na Helana alipokea taarifa ya mwanaye kuzama kwenye maji ambapo juhudi za kumtafuta zilifanikiwa kuupata mwili wake akiwa amepoteza maisha kabla ya siku chache baadaye mtoto wa mke mwenzake Evans Martin (2) kukutwa ndani ya shimo la choo masaa machache baada ya Helena kumpeleka kujisaidia.

Sauti ya Neema Maduhu Gedi (47) ambaye ni mama wa marehemu Evalin (10) akisimulia kifo cha mmwanaye na mtoto wa mke mwenziye alivyonusurika kwenye choo

Ikiwa bado familia inatafakari tukio la mtoto kutumbukia chooni, siku hiyo hiyo tarehe 12 July 2023 mida ya saa 11 jioni Julius Martin (6) alipotea nyumbani ambapo juhudi za kumtafuta kutoka kwa familia na wananchi wengine waliokutanishwa kwa njia ya yowe hazikuweza kuzaa matunda hadi mida ya usiku walipoazimia kwenda kupumzika.

Kesho yake zoezi la kutafuta liliendelea na mida ya saa 5:00 asubuhi walifanikiwa kuupata mwili wa mtoto huyo kando kando ya mlima ulio umbali wa mita 400 toka nyumbani kwao katika zoezi lililofanikishwa kwa asilimia kubwa na Helena jambo lililoongeza mashaka zaidi juu ya mgeni wao huyo waliyempokea tangu tarehe 27 Mei 2023 akitokea nchini Kenya kwa mama yake.

Ester Constantine Lukonge, Mama wa mtoto Evans aliyetumbukia chooni na Julius aliyekutwa amefariki mlimani akisimulia tukio

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtaa wa Nyamatoke, Sangi Mago Mahemba amesimulia mashaka waliyopata wananchi kuhusu maelezo ya Heleni juu ya namna alivyobaini mwili huo ambapo hatimaye jeshi la polisi liliondoka naye kwa uchunguzi zaidi.

Mwenyekiti mtaa wa Nyamatoke, Sangi Mago Mahemba akisimulia namna mwili wa mtoto Julius ulivyopatikana

Mazingira Fm amemtafuta Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mara, ACP Salum Ramadhani Morcase ambaye amethibitisha kutokea tukio hilo

Sauti ya Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mara, ACP Salum Ramadhani Morcase kuhusiana na tukio hilo