Storm FM
Storm FM
15 February 2026, 12:44 am

“Maendeleo ya kata yetu yanahitaji umoja na ushirikiano na tuweke makundi pembeni, na mimi nawahakikishia nitakuwa kiongozi wa wote bila kumbagua mtu” – Diwani Kulwa Ludaho
Na: Ester Mabula
Diwani wa Kata ya Ichwankima Kulwa Elias Ludaho iliyopo wilaya ya Chato katika jimbo la Chato kaskazini mkoani Geita, amefanya mkutano mkuu wa chama wa kata na wanachama wa CCM kwa lengo la kuwashukuru kwa kumchagua kutumikia kwa kipindi cha miaka mitano.
Akizungumza katika mkutano huo uliofanyika Februari 14, diwani huyo amewashukuru wanachama na wananchi kwa imani kubwa waliyoionesha kwake akieleza atawatumikia wote bila kuwa na ubaguzi.
Mgeni rasmi katika mkutano huo, Katibu wa CCM Wilaya ya Chato Dotto Mazuri, aliwahimiza wanachama kuendelea kudumisha umoja na mshikamano huku akiwahimiza wananchi kujiunga na mpango wa bima ya afya kwa wote unaotekelezwa na serikali ya awamu ya sita ili kujikinga na gharama kubwa za matibabu pindi wapatapo maradhi.

Katika hatua nyingine, mgeni maalumu ambaye ni mbaraza na diwani wa kata ya Kalangalala, Reuben Sagayika amechangia kiasi cha shilingi laki tatu kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya chama katika kata hiyo huku wajumbe waliohudhuria mkutano huo wakiahidi ushirikiano kwa diwani wa kata hiyo ili kuchochea maenedeleo.
Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi wa chama ngazi ya matawi, kijiji, kata na wilaya ambapo ulihitimishwa kwa viongozi waliofanya vizuri katika uchaguzi mkuu kwenye kata hiyo kupewa vyeti vya pongezi ambapo baadhi ya wajumbe wamempongeza diwani na kueleza wana matarajio makubwa ndani ya miaka mitano.
