Storm FM
Storm FM
13 February 2026, 12:02 pm

Shirika la THAMINI UHAI limepata ufadhili wa kutekeleza mradi wa Mama mjamzito na mtoto salama kwa muda wa miaka mitano kuanzia Septemba hadi Juni 2030 kupitia ufadhili wa pamoja wa Bloomberg Philanthropies na Gates Foundation.
Na: Ester Mabula
Shirika la THAMINI UHAI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na ofisi ya waziri mkuu, TAMISEMI linatarajia kutekeleza mradi wa Mama mjamzito na mtoto salama.
Mradi huo utatekelezwa katika mikoa ya Geita, Katavi na Kigoma ambapo unatarajiwa kusaidia katika kuimarisha huduma za kliniki ya wajawazito, huduma jumuishi za dharura za mama na mtoto ikijumuisha tiba kinga ya kutokwa damu baada ya kujifungua pamoja na matibabu ya watoto wachanga.
Kwa mkoa wa Geita utatekelezwa katika vituo vya afya viwili, Katoro na Bwanga, akizungumza jana Februari 12, 2026 katika uzinduzi wa mradi huo mkoani Geita, Mkurugenzi wa shirika la THAMINI UHAI Bw. Banzi Msumi hilo ameeleza mambo makuu yatakayotekelezwa katika mradi huo.

Mgeni rasmi, mkuu wa mkoa wa Geita Mhe. Martine Shigela amepongeza hatua ya kuwepo kwa mradi huo katika mkoa wa Geita akieleza kuwa utaleta tija pamoja na kuboresha huduma za afya huku mwakilishi kutoka ofisi ya waziri mkuu tamisemi , Idara ya afya, ustawi wa Jamii na Lishe Jesca Tryphone akisisitiza suala la uwajibikaji kwa watumishi wa idara ya afya ili kufikia malengo
Akizungumza baada ya zoezi la uzinduzi na kuutambulisha mradi huo mkoani Geita, Meneja miradi wa shirika la Thamini Uhai, Dkt. Sunday Dominiko amesema mradi huo una thamani ya dola za marekani milioni 12.15 ambapo utatekelezwa kwa muda wa miaka mitano.
