Storm FM

Kamati ya maendeleo kata ya Kalangalala yatembelea GGML

23 January 2026, 7:34 pm

Viongozi wa kata ya Kalangalala wakiwa katika moja ya mtambo (Dump truck) unaofanya shughuli ndani ya mgodi. Picha na Mpiga picha wetu

“Ziara hii imekuwa ni bora sana kwetu na yenye tija kwani itatuwezesha kuelewa kwa upana shughuli zinazofanyika ndani ya mgodi” – Diwani Sagayika

Na: Ester Mabula

Kamati ya maendeleo ya kata ya Kalangalala, halmashauri ya manispaa ya Geita ikiongozwa na Diwani wa Kata hiyo Reuben Emmanuel Sagayika, leo Januari 23, 2026, imefanya ziara maalumu ya kutembelea mgodi wa Geita Gold Mine (GGML) uliopo halmashauri ya manispaa ya Geita mkoani Geita.

Ziara hiyo imelenga kujifunza na kujionea shughuli mbalimbali za uchimbaji madini pamoja na mchango wa mgodi huo katika maendeleo ya jamii zinazouzunguka.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Diwani Sagayika amesema lengo kuu la kamati ni kupata uelewa wa kina kuhusu uendeshaji wa mgodi, fursa za ajira kwa wananchi wa eneo hilo, pamoja na miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR) inayotekelezwa na GGML.

Diwani wa kata ya Kalangalala Reuben Sagayika akizungumza wakati wa mafunzo maalumu (induction) yaliyotolewa kwa kamati hiyo. Picha na Mpiga picha wetu

Kwa upande wao, viongozi na wataalamu kutoka GGML waliipokea kamati hiyo na kutoa maelezo kuhusu historia ya mgodi, teknolojia zinazotumika katika uchimbaji wa madini, hatua za usalama kazini, pamoja na jitihada zinazochukuliwa kulinda mazingira.

Mtaalamu kutoka GGML akitoa maelezo kwa kamati ya juu ya shughuli zinazoendeshwa ndani ya GGML. Picha na Mpiga picha wetu

Ziara hiyo imeelezwa kuwa na manufaa makubwa kwa Kamati ya Maendeleo ya Kata ya Kalangalala, kwani itasaidia kutoa elimu sahihi kwa wananchi kuhusu shughuli za mgodi huo na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali ya kata na mgodi wa GGML kwa ajili ya maendeleo endelevu ya jamii.