Storm FM

Wazikimbia nyumba kisa moto wa ajabu Geita

15 January 2026, 4:39 pm

Baadhi ya Samani za ndani zilizotolewa nje kwa hofu ya moto. Picha na Ester Mabula

Ukistaajabu ya Mussa utayaona ya Firauni tukio hilo la kushangaza limewaacha wakazi wa mtaa huo katika hali ya taharuki.

Na Mrisho Sadick:

Moto wa ajabu umezikumba familia mbili katika mtaa wa Nyantorotoro Kata ya Nyankumbu Manispaa ya Geita Mkoani Geita huku wakazi wa eneo hilo wakiiomba serikali kuingilia kati kwani matukio hayo yamezua taharuki.

Wahanga wa tukio hilo wamelazimika kuzikimbia nyumba zao na kuanza kulala nje au kwa majirani kwa kuhofia usalama wa maisha yao, wakieleza kuwa moto huo umekuwa ukiwaka ghafla bila chanzo cha kawaida kinachofahamika.

Kutokana na hali hiyo, wameiomba serikali pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kuingilia kati sakata hilo, huku baadhi ya wakazi wakidai kuwa huenda chanzo cha matukio hayo kinahusishwa na imani za kishirikina, madai yaliyozidi kuongeza hofu na sintofahamu katika jamii.

Gari la zimamoto na uokoaji likiwa eneo la tukio la moto Nyantorotoro. Picha na Mrisho Sadick

Viongozi na wakazi wa mtaa wa Nyantorotoro wamesema matukio hayo yamewavuruga kisaikolojia na kuathiri maisha yao ya kila siku, wakisisitiza umuhimu wa kuchukuliwa hatua za haraka ili kuwahakikishia usalama wa wananchi na mali zao.

Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Geita Shabani Hamis Dawa akizungumzia tukio hili. Picha na Ester Mabula

Akizungumza kuhusu tukio hilo Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Geita Shabani Hamis Dawa amesema jeshi hilo limefika eneo la tukio na kuanza uchunguzi wa kina, akibainisha kuwa moto huo unaonekana kuwa wa ajabu na haujafanana na matukio ya kawaida ya moto nakwamba uchunguzi unaendelea kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama, huku akiwataka wananchi kuendelea kuwa watulivu, kutoa ushirikiano na kuepuka kueneza uvumi unaoweza kuongeza taharuki wakati serikali ikiendelea kufuatilia kwa karibu sakata hilo.

Sauti ya Ripoti ya Stori hii na Mrisho Sadick