Storm FM
Storm FM
5 September 2025, 1:11 am

Kituo hicho kitapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta huduma.
Na Kale Chongela:
Wakazi wa Kata ya Bukandwe wilayani Mbogwe mkoa wa Geita wanatarajia kuanza kunufaika na huduma za afya mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Kituo cha Afya cha Gakala kinachoendelea kujengwa katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Kituo hicho Bunga Dadu mradi huo unakadiriwa kugharimu shilingi bilioni tatu, na hadi sasa zaidi ya milioni 530 zimetumika amesema lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na za kibingwa karibu na makazi yao.

Mbio za Mwenge wa Uhuru zilipofika wilayani humo zimeweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa kituo hicho huku Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Ismail Ali Ussi ameridhishwa na mradi huo nakubainisha kuwa unakwenda sambamba na azma ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhamasisha Watanzania kutumia fursa za uwekezaji kwa maendeleo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe Sakina Mohamed amesema kituo hicho kitapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta huduma, kwani sasa idadi ya vituo imeongezeka kutoka saba hadi nane.